Vijana watakiwa kujiendeleza nje ya mfumo rasmi

Na. Lulu Luvanda, DODOMA

Jamii imetakuwa kuwahamasisha vijana waliokosa elimu katika mfumo rasmi kujiunga na Mpango wa Elimu Changamani kwa Vijana walio nje ya shule nchini Tanzania (IPOSA) ili kupata fursa ya kujiendeleza kielimu nje ya mfumo rasmi.



Akizungumza katika maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu wazima na nje ya mfumo rasmi yanayofanyika katika viwanja vya Nyerere square, Afisa Elimu ya Watu Wazima na Elimu Nje ya Mfumo Rasmi wa Elimu kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino, Annamaria Kidunda, alisema kuwa IPOSA inalenga kuwapa fursa vijana na wanafunzi ambao walishindwa kuendelea na mfumo rasmi wa elimu kupata nafasi nyingine ya kupata elimu nje ya mfumo rasmi.

Kwa mujibu wa Kidunda, IPOSA ni darasa linalowahusisha wanafunzi waliokatisha masomo au kushindwa kuendelea na mfumo rasmi wa elimu, kwa kuwawezesha kupata elimu na mafunzo yatakayowasaidia kukabiliana na mahitaji ya maisha ya sasa.

Alisema kuwa programu hiyo inalenga kuondoa pengo katika elimu kwa kuwapatia walengwa maarifa na stadi mbalimbali zitakazowawezesha kujitegemea, kuboresha maisha yao na kushiriki katika shughuli za maendeleo ya jamii. Mpango huo pia unatekelezwa kwa udhamini wa wadau wa UNICEF na Serikali ya Canada.

Kwa upande wa mnufaika ambae ni mwanafunzi wa IPOSA kutoka Wilaya ya Chamwino, Baraka Elias alisema kuwa elimu hiyo imemsaidia kupata maarifa ambayo amekuwa akiyatumia katika kuelimisha na kuielekeza jamii yake kuhusu umuhimu wa kutunza mazingira.

Alisema kuwa kupitia elimu aliyopata katika IPOSA, ameweza kuelewa kwa kina nafasi ya mtu binafsi katika kutunza mazingira na kuhamasisha jamii kuchukua hatua za kulinda mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Nae mwanafunzi na mnufaika wa IPOSA, Vestina Tumbi alisema kuwa mpango huo umemjengea uwezo wa kujitegemea kiuchumi baada ya kupata maarifa na ujuzi ambao umemsaidia kuanzisha na kuendesha biashara zake.

Maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu Wazima yanaendelea kutoa nafasi kwa wananchi na wadau mbalimbali kuelewa namna elimu nje ya mfumo rasmi inavyoweza kuwa daraja la kuwafikia vijana na watu ambao wamekosa fursa ya kuendelea na elimu katika mfumo wa kawaida yakiongozwa na kaulimbiu isemayo “Kisomo kwa Manufaa ya Watu, Dunia na Ustawi wa Jamii,”.

Comments

Popular Posts

Timu ya Watumishi Jiji la Dodoma inayoshiriki SHIMISEMITA yatakiwa kurejea na ushindi

Timu ya Watumishi Jiji la Dodoma waagwa kuelekea SHIMISEMITA

Dodoma Jiji yaifunga Mji Ifakara 41-3 Mpira wa Pete Mashindano ya SHIMISEMITA