Chuo Kikuu Huria chaungamkono kaulimbiu ya Kisomo kwa manufaa ya jamii

Na. Rahma Magona, DODOMA

 

Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kimeeleza namna kinavyotekeleza kaulimbiu ya Maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu Wazima na Elimu Nje ya Mfumo Rasmi kupitia programu mbalimbali zinazolenga kuwapatia wanafunzi maarifa na ujuzi wenye manufaa kwa watu, dunia na ustawi wa jamii.



Maelezo hayo yalitolewa leo tarehe 18 Agosti, 2026 katika maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu Wazima na Elimu Nje ya Mfumo Rasmi yanayofanyika katika Viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma.

Akizungumza katika banda la Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Afisa Udahili wa Chuo Kikuu Huria Tawi la Dodoma, Eliud Asajile alisema kuwa chuo hicho kinakwenda sambamba na kaulimbiu ya maadhimisho hayo kupitia programu zinazolenga kuandaa wanafunzi wenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya jamii. “Tuna programu kama ‘Certificate in Social Work’ inayotekeleza kaulimbiu ya ‘Kisomo kwa Manufaa ya Watu, Dunia na Ustawi wa Jamii’, kwa kumpa mwanafunzi maarifa ya kuwasiliana na jamii, kutambua mahitaji yake na kusaidia kuyafikia,” alisema Asajile.

Aliongeza kuwa kupitia programu hiyo, wanafunzi wanajengewa uwezo wa kutumia elimu wanayoipata katika kuisaidia jamii kwa kutambua changamoto na mahitaji yake na kushiriki katika kutafuta njia za kuyatatua.

Kwa upande wake mmoja wa wananchi waliotembelea banda la Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Nassor Juma alisema kuwa maadhimisho hayo yamemsaidia kufahamu zaidi kuhusu fursa za elimu zinazopatikana nje ya mfumo wa kawaida na namna elimu hiyo inavyoweza kumsaidia mtu kujiendeleza kielimu.

Ushiriki wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania katika maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu Wazima na Elimu Nje ya Mfumo Rasmi unaonesha nafasi ya elimu katika kuwawezesha wananchi kupata maarifa na ujuzi unaolenga kukidhi mahitaji ya jamii, huku ukisisitiza umuhimu wa kujifunza kwa maendeleo na ustawi wa jamii.

Comments

Popular Posts

Timu ya Watumishi Jiji la Dodoma inayoshiriki SHIMISEMITA yatakiwa kurejea na ushindi

Timu ya Watumishi Jiji la Dodoma waagwa kuelekea SHIMISEMITA

Dodoma Jiji yaifunga Mji Ifakara 41-3 Mpira wa Pete Mashindano ya SHIMISEMITA