Jiji la Dodoma Biashara saa 24, usafi saa 24
Na. Mwandishi wetu, MSALATO Wananchi wa Jiji la Dodoma wametakiwa kuendesha biashara saa 24 huku wakihakikisha usafi wa mazingira unafanyika muda wote, ili huduma ziendelee kupatikana bila kuathiri usafi wa maeneo yao. Rai hiyo imetolewa wakati wa Uzinduzi wa Kampeni Endelevu ya Usafi wa Mazingira katika eneo la Mnada wa Msalato, jijini Dodoma, ambapo ilisisitizwa kuwa dhana ya “biashara saa 24” inapaswa kwenda sambamba na “usafi saa 24.” Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri alisema kuwa maafisa afya pamoja na watendaji wa kata na mitaa watakuwa wakifanya ukaguzi wa mara kwa mara katika maeneo ya biashara ili kuhakikisha usafi unazingatiwa muda wote. “Biashara masaa 24, lakini usafi masaa 24. Maafisa afya, watendaji wa kata na mitaa watakuwa wakipita kufanya ukaguzi, na atakayekaidi maelekezo ya usafi atatozwa faini ya shilingi 50,000 hadi shilingi 300,000,” alisema Alhaj Shekimweri. ...