Kliniki ya Kata ya Kikuyu Kaskazini kuwasogezea huduma wananchi mlangoni
Na. Leah Mabalwe, DODOMA Wananchi wa Kata ya Kikuyu Kaskazini Jijini Dodoma wanatarajiwa kunufaika na huduma mbalimbali za serikali kupitia Kliniki ya Kata itakayoanzishwa wiki hii ikiwa ni hatua ya kusogeza huduma karibu na wananchi na kuwawezesha kupata huduma mbalimbali kwa urahisi. Hayo aliyazungumza Diwani wa Kata ya Kikuyu Kaskazini, Herry Beji nje ya ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma. Alisema kuwa Kliniki hiyo itafanyika kwa muda wa wiki moja katika Shule ya Msingi Kikuyu, ambapo idara na taasisi mbalimbali zitashiriki katika kutoa huduma kwa wananchi, miongoni mwa huduma zitakazopatikana ni huduma za ardhi. “Lengo letu ni kusogeza huduma karibu na wananchi ili wasipate usumbufu wa kwenda katika ofisi mbalimbali kutafuta huduma, ambapo wataalamu kutoka seksheni ya Ardhi ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma pamoja na Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Mkoa wa Dodoma watakuwepo kusikiliza na kushughulikia changamoto mbalimbali za wananchi zinazohusu masuala ya Ardhi ...