Mwenyekiti Mtaa wa Karume, Kata ya Mnadani ahamasisha usafi
Na. Mwandishi wetu, MNADANI
Zoezi la usafi wa mazingira limehamasishwa katika Mtaa
wa Karume, Kata ya Mnadani, kwa lengo la kuimarisha usafi na afya ya wananchi
pamoja na kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kutunza mazingira.
Zoezi hilo pia limehusisha wataalam wa Kanda Namba Sita, ambao wamekuwa mstari wa mbele kutoa elimu na ushauri kwa wananchi kuhusu umuhimu wa usafi wa mazingira, utunzaji wa taka na namna ya kuzuia magonjwa yanayoweza kusababishwa na mazingira machafu.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Mwenyekiti wa Mtaa
wa Karume, Waziri Matwiga amewataka wananchi kushiriki kikamilifu katika usafi
wa mazingira na kujenga utamaduni wa kufanya usafi mara kwa mara.
“Usafi wa mazingira ni jukumu la kila mmoja wetu.
Tunapaswa kushirikiana kuhakikisha mtaa wetu unakuwa safi na salama kwa afya ya
wananchi,” amesema Matwiga.
Kwa upande wao, wataalam wa Kanda Namba Sita wameendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kutunza mazingira, ikiwa ni pamoja na kuepuka kutupa taka hovyo, kuhakikisha taka zinakusanywa na kuwekwa katika maeneo yanayostahili, pamoja na kuzingatia usafi wa maeneo ya makazi na maeneo ya huduma za jamii.
Wataalam hao wamesisitiza kuwa usafi wa mazingira ni
sehemu muhimu ya kinga dhidi ya magonjwa na unahitaji ushiriki wa wananchi,
viongozi na wadau mbalimbali kwa pamoja.
Comments
Post a Comment