Diwani Kata ya Miyuji azindua kampeni ya usafi wa Mazingira
Na. Mwandishi wetu, MIYUJI
Diwani wa Kata ya Miyuji, Ringo Iringo, amezindua
kampeni ya usafi wa mazingira kwa kushirikiana na wataalamu wa Kanda Namba Sita
huku akiwataka wananchi kushiriki kikamilifu katika kuhakikisha mazingira
yanakuwa safi na salama.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo, Iringo amesema kuwa usafi wa mazingira ni jukumu la kila mwananchi na kwamba juhudi za pamoja zinahitajika ili kukabiliana na changamoto ya uchafu katika maeneo ya makazi na maeneo ya wazi.
“Nawasihi wananchi wote tushirikiane katika kuhakikisha
mazingira yetu yanakuwa safi. Usafi ni msingi wa afya bora na maendeleo ya
jamii,” amesema Iringo.
Amesema kuwa kampeni hiyo inalenga kuhamasisha
wananchi kuwa na utamaduni wa kufanya usafi mara kwa mara, kutunza maeneo yao
na kuepuka kutupa taka hovyo.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mtaa wa Miyuji Proper, Hawad Mbogela, amewataka wananchi kuunga mkono kampeni hiyo na kuhakikisha usafi unaendelea kuwa sehemu ya maisha ya kila siku.
“Tunaomba wananchi wote tushirikiane na viongozi
katika kutunza mazingira. Zoezi hili lisibaki kuwa la siku moja; kila mmoja
anatakiwa kuhakikisha eneo analoishi na kulizunguka linakuwa safi,” amesema
Mbogela.
Mbogela amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya wananchi
na viongozi ni muhimu katika kuhakikisha kampeni ya usafi inakuwa endelevu na
kuleta matokeo chanya kwa jamii.
Uzinduzi wa kampeni hiyo umejikita katika kuhamasisha
wananchi wa Kata ya Miyuji kuhusu umuhimu wa usafi, utunzaji wa mazingira na
uwajibikaji wa pamoja katika kujenga jamii yenye mazingira safi na salama.
Comments
Post a Comment