Jiji la Dodoma lapongezwa kukusanya zaidi ya 100% mapato ya ndani Mwaka wa Fedha 2025/2026
Na. Leah Mabalwe, DODOMA
Halmashauri ya Jiji la Dodoma yapongezwa kwa namna
inavyosimamia na kukusanya mapato, hatua inayochangia kwa kiasi kikubwa
utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika jiji hilo kufuatia ukusanyaji wa zaidi ya asilimia 100 kwa bajeti ya mwaka 2025/2026.
Pongezi hizo zilitolewa na Mbunge wa Viti Maalum, Aisha Msantu mara baada ya kusomwa kwa taarifa ya tathmini ya mapato kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026, katika Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Dodoma lililofanyika katika ukumbi wa halmashauri hiyo.
Alisema kuwa juhudi zinazoendelea kufanywa na halmashauri
katika ukusanyaji na usimamizi wa mapato zinapaswa kupongezwa, huku akisisitiza
umuhimu wa kuendelea kusimamia vyanzo vya mapato kwa ufanisi ili kuwezesha
utekelezaji wa bajeti na mipango ya maendeleo ya jiji. “Nipende kuwapongeza halmashauri
kwa namna ambavyo wanaendelea kukusanya na kusimamia mapato. Lakini pia katika
utekelezaji wa bajeti ya jiji kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026, tunaona juhudi
kubwa zinazofanyika hadi kufikia ukusanyaji mapato wa zaidi ya asilimia 100” alisema Msantu.
Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Mnadani, Mgendi
Kerenge alisema kuwa ukusanyaji wa mapato unaofanywa na Halmashauri ya Jiji la
Dodoma unaendelea kuleta matokeo chanya kwa wananchi, kwasababu sehemu ya
mapato hayo inaonekana kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali katika kata.
“Halmashauri ya Jiji la Dodoma inaendelea kukusanya mapato, lakini kupitia mapato haya ndiyo tunayoona maendeleo katika kata zetu. Shule zinajengwa, hospitali zinajengwa na maendeleo mbalimbali yanafanyika katika kata zetu kupitia mapato haya haya yanayokusanywa, maendeleo yanayoonekana katika maeneo mbalimbali ya jiji yanatokana kwa kiasi kikubwa na mapato yanayokusanywa na halmashauri, ambayo huwezesha utekelezaji wa miradi muhimu ya kijamii na kiuchumi” alisema Kerenge.
Alisema kuwa ni muhimu wananchi kuendelea kushirikiana
na halmashauri katika kuhakikisha wanatimiza wajibu wao wa kulipa kodi na tozo
mbalimbali kwa wakati, kwa kuwa mapato hayo ndiyo msingi wa utekelezaji wa
huduma na miradi ya maendeleo inayowagusa wananchi moja kwa moja.
Kwa ujumla, viongozi hao wameeleza kuwa kuimarika kwa
ukusanyaji na usimamizi wa mapato ni hatua muhimu katika kuhakikisha
Halmashauri ya Jiji la Dodoma inaendelea kutekeleza mipango yake ya maendeleo
na kuboresha huduma kwa wananchi.
Comments
Post a Comment