Kliniki ya Kata ya Kikuyu Kaskazini kuwasogezea huduma wananchi mlangoni
Na. Leah Mabalwe, DODOMA
Wananchi wa Kata ya Kikuyu Kaskazini Jijini Dodoma
wanatarajiwa kunufaika na huduma mbalimbali za serikali kupitia Kliniki ya Kata
itakayoanzishwa wiki hii ikiwa ni hatua ya kusogeza huduma karibu na wananchi
na kuwawezesha kupata huduma mbalimbali kwa urahisi.
Hayo aliyazungumza Diwani wa Kata ya Kikuyu Kaskazini, Herry Beji nje ya ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.
Alisema kuwa Kliniki hiyo itafanyika kwa muda wa wiki
moja katika Shule ya Msingi Kikuyu, ambapo idara na taasisi mbalimbali
zitashiriki katika kutoa huduma kwa wananchi, miongoni mwa huduma
zitakazopatikana ni huduma za ardhi. “Lengo letu ni kusogeza huduma karibu na
wananchi ili wasipate usumbufu wa kwenda katika ofisi mbalimbali kutafuta
huduma, ambapo wataalamu kutoka seksheni ya Ardhi ya Halmashauri ya Jiji la
Dodoma pamoja na Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Mkoa wa Dodoma watakuwepo
kusikiliza na kushughulikia changamoto mbalimbali za wananchi zinazohusu
masuala ya Ardhi na taasisi nyingine
moja kwa moja katika Kata ya Kikuyu Kaskazini” alisema Beji.
Diwani huyo alizitaja huduma nyingine zitakazotolewa
kutoka taasisi za DUWASA, TANESCO, Idara ya Afya, NIDA pamoja na taasisi
nyingine, ambazo zitapata fursa ya kutoa huduma na kusikiliza changamoto za
wananchi katika eneo moja.
Kwa upande wake, Mbunge wa Viti Maalum, Aisha Msantu,
aliwataka madiwani kuendelea kuwa karibu na wananchi na kusimamia mahitaji
pamoja na changamoto zinazowakabili katika maeneo yao ili kuhakikisha
yanapatiwa ufumbuzi kwa wakati. “Ni muhimu kuendelea kusikiliza kero za
wananchi, ninawasihi madiwani muendelee kuwa karibu na wananchi, msikilize
mahitaji yao na muendelee kuyasimamia mpaka yapate majibu. Mwananchi anahitaji
kuona kiongozi wake yupo pamoja naye na anasimamia changamoto zinazomkabili” alisema
Msantu.
Kliniki ya Kata ni fursa muhimu kwa wananchi kupata
huduma mbalimbali kwa wakati mmoja, hivyo wananchi wote wa Kata ya Kikuyu
Kaskazini kujitokeza kwa wingi katika Shule ya Msingi Kikuyu ili kupata huduma,
ushauri na ufumbuzi wa changamoto zao kutoka kwa taasisi na idara mbalimbali
zitakazoshiriki.
Comments
Post a Comment