Kata ya Ihumwa yaanza usafi kutekeleza agizo la RC Dodoma

Na. Rahma Magona, DODOMA

Kata ya Ihumwa katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma imeanza zoezi la usafi wa mazingira ikiwa ni hatua ya utekelezaji wa maagizo ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule ya kuhakikisha wananchi wanaimarisha usafi wa mazingira na kulinda afya zao.


 

Hatua hiyo imekuja baada ya viongozi wa Kata ya Ihumwa kuanza kuhamasisha wananchi kufanya usafi mtaa kwa mtaa kwa kushirikiana na maafisa afya kutoka Kanda Namba Mbili, huku ukaguzi wa vyoo katika kaya ukiwa miongoni mwa hatua zinazotekelezwa.

 

Akizungumza katika zoezi hilo, Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Chang’ombe, Kata ya Ihumwa, Yoram Ndumizi alisema kuwa wamejipanga vizuri kuhakikisha wananchi wanashiriki katika usafi huku wakifanya ukaguzi wa vyoo baada ya kubaini baadhi ya kaya kutokuwa na vyoo, hali hiyo inaweza kuongeza hatari ya mlipuko wa magonjwa kutokana na uwezekano wa mvua nyingi za El NiƱo.

 

Ndumizi aliongeza kuwa kwa kushirikiana na maafisa afya, wanaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa usafi wa mazingira na namna unavyoweza kusaidia kuzuia magonjwa ya kuambukiza.

 

Nae, mkazi wa Kata ya Ihumwa, Onesmo Jonas alisema kuwa usafi wa mazingira una umuhimu mkubwa katika kulinda afya za wananchi, akieleza kuwa moja ya faida za kuzingatia usafi ni kuepukana na magonjwa mbalimbali ikiwemo kipindupindu.

 

Kata ya Ihumwa imeendelea kuhamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika zoezi la usafi na kuhakikisha kila kaya inazingatia usafi wa mazingira pamoja na kuwa na vyoo bora, hatua inayolenga kuzuia milipuko ya magonjwa na kulinda afya za wananchi.

Comments

Popular Posts

Kata ya Miyuji Yaongeza Kasi ya Usimamizi Wa Usafi wa Mazingira

Kata za Nkuhungu na Kizota zajiandaa kukabiliana na mvua za El Nino

Wafanyabiashara Soko la Miembeni Waazimia Kulinda Usafi