Zoezi la Kuua Mbwa Wanao Zurura Lafanyika Kata ya Msalato

Na. Manase Malima, MSALATO

 

Zoezi la kuua mbwa wanao zurura limefanyika katika Kata ya Msalato, Halmashauri ya Jiji la Dodoma, likihusisha maeneo ya Machinjioni, Magereza na Mnadani, kutokana na kero na hatari zinazowakabili wananchi ambapo mbwa zaidi ya 20 waliuliwa.



Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Afisa Mifugo wa Kanda Namba Sita ya utoaji huduma Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Prisca Mottee alisema kuwa mbwa hao wamekuwa wakisababisha usumbufu kwa wananchi, wakiwemo watoto na wanafunzi wanaokwenda na kurudi shuleni, Afisa Mifugo kanda Namba Sita aliongeza kuwa zoezi hilo ni endelevu na litafanyika katika maeneo mengine yenye changamoto hiyo, huku akiwataka wafugaji kuwafungia mbwa wao na kuzingatia kuwapatia chanjo.

Kwa upande wake Afisa Mifugo Kata ya Msalato, Maisha Jiwa alisema kuwa hatua hiyo imechukuliwa kufuatia malalamiko ya wananchi kuhusu mbwa wanao zurura katika maeneo mbalimbali ya kata hiyo.

“Kumekuwa na adha kubwa ya mbwa wanaozurura katika maeneo ya Machinjioni, Mnadani na kwenye makazi ya wananchi. Wanafunzi wamekuwa wakitishwa na kufukuzwa wanapokwenda au kurudi shule, huku baadhi ya wananchi, wakiwemo watoto, wakiripotiwa kung’atwa na mbwa hao. Kwa hiyo tumeanza kuchukua hatua ya kuwaondoa na zoezi hili litaendelea katika maeneo yote yenye changamoto,” alisema Jiwa.

Jiwa alisisitiza kuwa zoezi hilo pia limehusisha maeneo ambayo wananchi walitoa taarifa kuhusu usumbufu unaosababishwa na mbwa wazururaji, ikiwemo eneo la Magereza. Alisema kuwa hatua hiyo inalenga kupunguza hatari na kurejesha usalama wa wananchi, hasa watoto wanaotumia njia hizo wakati wa kwenda na kurudi shuleni.

Kwa upande wake, mkazi wa Kata ya Msalato, Godfrey David, alisema kuwa zoezi hilo ni muhimu kwa kuwa mbwa hao wamekuwa wakisababisha usumbufu kwa wanafunzi na wananchi, hasa wakati wa asubuhi na katika eneo la Mnadani. Amesema serikali kuchukua hatua hiyo ni jambo zuri na amewataka wafugaji kuhakikisha wanawafunga mbwa wao na kuhakikisha hawazururi mitaani.

Zoezi hilo ni sehemu ya hatua zinazoendelea kuchukuliwa katika Kata ya Msalato kukabiliana na mbwa wazururaji na kupunguza madhara kwa wananchi. Wafugaji wa mbwa wametakiwa kuwafungia, kuwapatia chanjo na kuhakikisha wanawafuga kwa kuzingatia usalama wa jamii.

 

Comments

Popular Posts

Kata ya Miyuji Yaongeza Kasi ya Usimamizi Wa Usafi wa Mazingira

Kata za Nkuhungu na Kizota zajiandaa kukabiliana na mvua za El Nino

Mwenyekiti Mtaa wa Karume, Kata ya Mnadani ahamasisha usafi