Usafi wa mitaro na njia za maji Kusaidia kujikinga na mafuriko Dodoma Makulu

Na. Amoni Sambulila, DODOMA

 

Wito umetolewa kwa wananchi kuhakikisha mitaro na njia za maji zinakuwa safi na wazi wakati wote, ili kuruhusu maji ya mvua kupita kwa urahisi na kuzuia maji kufurika na kuingia kwenye makazi ya wananchi.

 


Wito huo umetolewa na Kaimu Meneja wa Kanda Namba Nne, Evodius Canisto wakati wa zoezi la usafi wa mazingira lililofanyika katika kata hiyo ambapo aliwataka wananchi kufanya usafi katika maeneo yote yanayoweza kuathiriwa na maji ya mvua.

 

Evodius alisema kuwa mabadiliko ya tabianchi yanaweza kusababisha mvua kubwa na kwa nyakati tofauti hivyo wananchi wanapaswa kuchukua hatua mapema kwa kusafisha mitaro, kuondoa taka na vitu vingine vinavyoweza kuziba njia za maji.

 

Aliongeza kuwa usafi wa mazingira ni jukumu la kila mwananchi na haupaswi kufanyika wakati wa zoezi maalum pekee bali inapaswa kuwa sehemu ya maisha ya kila siku ili kulinda afya, usalama na mali za wananchi.

 


Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Shina eneo la Mkalama, Chalesi Jacobo amewataka wananchi kuendelea kushiriki katika usafi wa mazingira akisisitiza umuhimu wa kuhakikisha mitaro inasafishwa mara kwa mara.

 

Nae, Mwenyekiti wa Shina Namba Mbili, Paulo Ainea alisema kuwa wananchi wanapaswa kuwa na utamaduni wa kufanya usafi katika maeneo yao bila kusubiri kuhamasishwa kwasababu hatua hiyo inaweza kusaidia kupunguza athari za mafuriko wakati wa mvua zinazotarajiwa kunyesha kwa wingi.

 

Zoezi hilo limefanyika katika Kata ya Dodoma Makulu likilenga kuhamasisha wananchi kuimarisha usafi wa mazingira na kujiandaa mapema kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mabadiliko ya tabianchi.






Comments

Popular Posts

Kata ya Miyuji Yaongeza Kasi ya Usimamizi Wa Usafi wa Mazingira

Kata za Nkuhungu na Kizota zajiandaa kukabiliana na mvua za El Nino

Wafanyabiashara Soko la Miembeni Waazimia Kulinda Usafi