CCTV Camera zaimarisha usalama Jiji la Dodoma

Na. Mwandishi wetu, DODOMA

 

Ufungaji wa kamera za CCTV katika maeneo mbalimbali umeendelea kuimarisha usalama, utii wa sheria za barabarani na ulinzi katika Jiji la Dodoma, huku madiwani wakipokea taarifa ya utendaji kazi wa TEHAMA.

 


Kauli hiyo ilitolewa na Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Vincent Oderо wakati akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 katika mkutano wa Mwaka wa Baraza la Madiwani uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa jiji hilo.

 

Alisema kuwa Mwaka wa Fedha 2024/2025, maeneo 35 yalipangwa kufungwa kamera za CCTV, ambapo manne yalifungwa na maeneo 31 yakabaki kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026, maeneo 31 yalipangwa kufungwa CCTV, ambapo 26 yamekamilika na maeneo matano bado hayajafungwa.

 

“Katika utekelezaji wa mifumo ya TEHAMA, kwa mwaka wa fedha 2024/2025, taasisi 287 kati ya 333 zilizopangwa zilifungiwa mifumo. Kwa mwaka wa fedha 2025/2026, taasisi 179 kati ya 227 zilizopangwa zimefungiwa mifumo. Hatua hizi zinaendelea kuongeza matumizi ya teknolojia,” alisema Onderо.

 

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Zuzu, Jenesta Malingo, alisema kuwa uwepo wa CCTV kamera barabarani unasaidia wananchi kufuata sheria bila kulazimishwa, huku ukirahisisha ufuatiliaji na udhibiti wa matukio yanayoweza kuhatarisha amani na usalama.

 

Alisema kuwa Dodoma ina umuhimu wa kipekee kutokana na kuwa Makao Makuu ya nchi, ambako kuna Bunge, viongozi mbalimbali wa kitaifa na Ikulu, hivyo matumizi ya TEHAMA ni muhimu katika kuimarisha ulinzi na usalama.

 

“Naipongeza serikali, uongozi wa jiji na watendaji wa Kitengo cha TEHAMA kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya katika kuhakikisha matumizi ya teknolojia yanaimarika. Uwepo wa mifumo ya TEHAMA na kamera za CCTV umeongeza ufanisi katika ulinzi na usalama na kuifanya Dodoma kuwa jiji la kisasa,” alisema Malingo.

 

Madiwani walipokea taarifa hiyo ya utendaji kazi wa halmashauri, ikiwemo utekelezaji wa shughuli za Kitengo cha TEHAMA katika Miaka ya Fedha 2024/2025 na 2025/2026, huku wakielezwa hatua zilizochukuliwa katika kuimarisha mifumo ya kidijitali, usalama na matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Kata ya Miyuji Yaongeza Kasi ya Usimamizi Wa Usafi wa Mazingira

Kata za Nkuhungu na Kizota zajiandaa kukabiliana na mvua za El Nino

Zoezi la Kuua Mbwa Wanao Zurura Lafanyika Kata ya Msalato