GCU Jiji la Dodoma yapongezwa umahiri katika kuhabarisha Umma
Na. Mwandishi wetu, DODOMA
BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Dodoma
limekipongeza Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kwa kazi nzuri ya kuhakikisha
wananchi wanapata taarifa na habari kuhusu shughuli na utekelezaji wa majukumu
ya halmashauri kwa wakati.
Pongezi hizo zilitolewa na Diwani wa Kata ya Mnadani, Mugendi Kerenge wakati akichangia kwenye mkutano wa Baraza la Madiwani kwa ajili ya kupokea na kuajdili taarifa ya utekelezaji wa kazi za halmashauri kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026, uliofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.
Kerenge aliwapongeza wataalam wa Kitengo cha
Mawasiliano Serikalini kwa namna walivyokuwa wakitekeleza majukumu yao ya
kuhabarisha umma kuhusu shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na halmashauri.
“Nawapongeza wataalam wetu wa habari kwa namna
wanavyofanya kazi nzuri ya kuhabarisha umma kwa wakati. Wananchi wamekuwa
wakipata habari mbalimbali kutoka katika maeneo yao. Mfano, mimi habari za kata
yangu zimekuwa zikitolewa mara nyingi na kwa wakati hivyo kuwawezesha wananchi
kufahamu kinachoendelea na mikakati tuliyonayo” alisema Kerenge.
Kwa upande wake, Afisa Habari katika Halmashauri ya
Jiji la Dodoma, Leah Mabalwe alisema kuwa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
kina jukumu la kuhakikisha wananchi wanapata taarifa, habari na matangazo
mbalimbali ya halmashauri kwa wakati ili wawe na uelewa wa kila jambo
linalotekelezwa na serikali yao.
Mabalwe alisema kuwa kitengo hicho kitaendelea
kushirikiana na viongozi na wataalam wa halmashauri katika kuhakikisha wananchi
wanafahamishwa kwa usahihi na kwa wakati kuhusu shughuli za maendeleo, huduma
na fursa zinazotolewa na halmashauri.
Alisema kuwa kuimarishwa kwa mawasiliano kati ya halmashauri
na wananchi kutaendelea kuwa sehemu muhimu ya kuhakikisha umma unapata taarifa
sahihi, kwa wakati na kupitia njia rasmi za mawasiliano za halmashauri.
Comments
Post a Comment