Ufaulu Elimu Sekondari wapanda Jiji la Dodoma
Na. Mwandishi wetu, DODOMA
Ufaulu wa mitihani ya taifa kwa wanafunzi wa sekondari
Jiji la Dodoma umeimarika kwa Mwaka 2025/2026, ambapo Division I, II na III
zikiongezeka.
Hayo yameelezwa na Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Vincent Odero wakati akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 katika Mkutano wa Mwaka wa Baraza la Madiwani uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa jiji hilo.
Alisema kuwa mwelekeo huo unaashiria maendeleo chanya
katika sekta ya elimu ya sekondari, yakichangiwa na usimamizi mzuri wa elimu
pamoja na juhudi kubwa za walimu katika kuboresha ufundishaji na kuongeza
ufaulu wa wanafunzi.
“Wanafunzi waliofanya mtihani waliongezeka kutoka
6,526 Mwaka 2024/2025 hadi 7,104 Mwaka 2025/2026, huku ufaulu wa ‘Division’ I,
II na III ukiongezeka na ‘Division’ 0 na IV ukipungua. Hii inaashiria mwelekeo
chanya unaoendelea,” alisema Odero.
Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Viwandani, Swalihina
Athuman alisema kuwa walimu wamekuwa na mchango mkubwa katika kuongeza ufaulu
kwa kuwapatia wanafunzi muda wa ziada wa masomo na kuendesha kambi za masomo.
Alisema kuwa ushirikiano wa wazazi, walimu na Baraza
la Madiwani umeendelea kuwa muhimu katika kusimamia maendeleo ya wanafunzi,
huku wazazi wakihimizwa kuongeza ufuatiliaji wa watoto wanapokuwa nyumbani ili
kuimarisha zaidi ufaulu.
“Tunatoa pongezi kwa walimu. Walimu wamefanya juhudi
kubwa, wameongeza mazingira mazuri ya ufaulu kwa watoto kwa kutoa muda wao wa
kuwasomesha na kuwafanya watoto wale wawe wanarejea mara kwa mara,” alisema
Athuman.
Jiji la Dodoma lina jumla ya shule 72 za sekondari,
zikiwemo shule 46 za serikali na shule 26 za binafsi, zenye wanafunzi 45,692.
Kati yao, wanafunzi 38,839 wanasoma katika shule za serikali, wakiwemo wavulana
17,167 na wasichana 21,672, huku shule za binafsi zikiwa na wanafunzi 6,853,
wakiwemo wavulana 3,656 na wasichana 3,197.
MWISHO
Comments
Post a Comment