Wakulima wahimizwa kupanda Marigold kufukuza wadudu shambani

Na. Mwandishi wetu, NZUGUNI

Wakulima wa vipando bustani katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma wametakiwa kutumia maua aina ya Marigold kama njia ya asili ya kudhibiti wadudu na kuboresha mazingira ya mashamba, hatua inayolenga kupunguza matumizi ya dawa za viwandani katika kilimo.


Ua aina ya Marigold

Akizungumza katika maonesho ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Dkt. John Malecela Afisa Kilimo wa jiji hilo, Fatuma Doow alisema kuwa matumizi sahihi ya maua ya Marigold ni sehemu muhimu ya kuboresha afya ya mashamba na bustani kwa kuongeza thamani ya mandhari ya maeneo ya kilimo.

Alisema kuwa maua ya Marigold yanapandwa pembezoni mwa vipando vya bustani na husaidia kuongeza urembo, sambamba na kusaidia kuzuia na kufukuza baadhi ya wadudu wanaoweza kuhamia kutoka katika mashamba mengine.

“Ushauri wangu kwa wakulima wa mazao ya bustani ni kupanda maua pembezoni mwa mazao hayo ili kusaidia kupunguza matumizi ya dawa za wadudu na kuimarisha matumizi ya njia rafiki kwa mazingira katika udhibiti wa wadudu,” alisema Doow.

Kwa upande wake, mdau na mfanyabiashara wa Maua katika Jiji la Dodoma, Monica Mhina alisema kuwa sekta ya maua ina fursa kubwa kutokana na kuongezeka kwa uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa mimea ya mapambo katika kuboresha mazingira na maisha ya kila siku.


Ua aina ya Ulimi wa Mama Mkwe


“Kuna maua ya aina mbalimbali yenye faida tofauti, lakini Ulimi wa mama mkwe husaidia kuboresha hewa ndani ya nyumba, Saigonia hupendezesha mazingira na husaidia kupunguza mawazo. Pia, watu wengi hupenda ‘money tree’ kutokana na imani kwamba huleta mafanikio na ustawi. Ninawashauri wananchi wenzangu kupanda maua kwa sababu yana faida nyingi zaidi ya urembo,” alisema Mhina.

Nae, mkazi wa Jiji la Dodoma aliyefika kutembelea maonesho hayo kwa ajili ya kujifunza, Asha Mwakalobo alisema kuwa amepata maarifa mapya kuhusu umuhimu wa maua katika maisha ya kila siku.

“Nilikuwa najua maua ni kwa ajili ya urembo tu, lakini leo nimejifunza kwamba mengine yanaweza kusaidia kupunguza wadudu mashambani na kuboresha hewa ndani ya nyumba. Nimepata hamasa ya kuanzisha bustani ndogo nyumbani kwangu,” alisema Mwakalobo.


Ua aina ya Saigonia husaidia kuondoa stress


Maonesho ya Nanenane yameendelea kuwa jukwaa la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu teknolojia, ubunifu na mbinu mbalimbali za kuboresha uzalishaji wa kilimo pamoja na utunzaji wa mazingira. 

Comments

Popular Posts

Barabara za Mtaa wa Mbwanga yafunguliwa, Diwani Kerenge aitaja kuwa chachu ya maendeleo

Kanda Namba Tatu yaimarisha ushirikiano na wamiliki wa vituo vya malezi ya watoto Dodoma

BANDA YA JIJI LA DODOMA LATOA TEKNOLOJIA UFUGAJI SAMAKI NA KUKU PAMOJA