Matenga yageuka lulu kilimo cha mbogamboga Dodoma

Na. Mwandishi wetu, NZUGUNI

Wananchi wanaoishi mijini, hususan kwenye nyumba za kupanga wametakiwa kutumia matenga, makopo ya maji na matairi yaliyotumika kuanzisha bustani za mbogamboga majumbani ili kujihakikishia upatikanaji wa chakula salama, kupunguza gharama za maisha na kuhifadhi mazingira.



Wito huo ulitolewa na Afisa Kilimo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Zaidina Juma wakati wa maonesho ya 32 ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Malecela mjini Dodoma.

Alisema kuwa kilimo cha kwenye matenga ni njia rahisi inayosaidia kuhifadhi mazingira huku kikitatua changamoto ya upatikanaji wa maeneo ya kulima.

Alisema kuwa wananchi wengi wanaishi kwenye nyumba za kupanga au maghorofani ambako hakuna nafasi ya kuanzisha bustani za kawaida, lakini bado wanaweza kuzalisha mboga zao kwa kutumia vifaa vinavyotupwa na kula mboga zenye usalama, tofauti na baadhi ya mazao yanayouzwa sokoni ambayo wakati mwingine huvunwa muda mfupi baada ya kunyunyiziwa viuatilifu.

 “Ukilima nyumbani unakuwa na uhakika wa kile unachokula, kwa sababu unajua namna ulivyokizalisha na huna wasiwasi wa kemikali zinazoweza kubaki kwenye mboga. Badala ya kutupa makopo, matairi au matenga, vitumike kuzalisha chakula. Hii ni njia ya kuhifadhi mazingira na wakati huohuo, kuongeza usalama wa chakula kwenye kaya,” alisema Juma.

Kwa upande wake Mdau wa Kilimo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Juma Mtega alisema kuwa bustani za kwenye matenga ni suluhisho linalokwenda sambamba na ukuaji wa miji, kwasababu zinawawezesha wananchi kuzalisha chakula hata katika maeneo yenye nafasi ndogo.

“Leo watu wengi wanaishi kwenye nyumba za kupanga na viwanja vidogo. Teknolojia hii inawapa fursa ya kujitosheleza kwa mboga, kupunguza matumizi ya fedha na kuongeza lishe kwa familia,” alisema Mtega.

Nae, mkazi wa Kata ya Chang’ombe Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Asha Hamis anayeishi katika nyumba ya kupanga alisema kuwa maonesho hayo yamempa hamasa na fursa ya kujifunza kilimo cha mjini ambacho hakina gharama kubwa katika kukianzisha.

“Nimeona kumbe si lazima uwe na shamba. Nikipata matenga mawili au matatu na kupanda mboga zangu, nitapunguza gharama za kununua mboga kila siku na nitakuwa na uhakika wa ubora wake,” alisema Hamis.

Comments

Popular Posts

Barabara za Mtaa wa Mbwanga yafunguliwa, Diwani Kerenge aitaja kuwa chachu ya maendeleo

Kanda Namba Tatu yaimarisha ushirikiano na wamiliki wa vituo vya malezi ya watoto Dodoma

BANDA YA JIJI LA DODOMA LATOA TEKNOLOJIA UFUGAJI SAMAKI NA KUKU PAMOJA