Dodoma yazalisha Bayogesi kulinda utunzaji wa Mazingira na matumizi ya Nishati safi

Na. Mwandishi wetu, DODOMA

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imeendelea kuonesha dhamira yake ya kulinda mazingira kwa kuhamasisha matumizi ya nishati safi kupitia uzalishaji wa bayogesi (Biogas) inayotokana na kinyesi cha mifugo na mabaki ya chakula ikiwa ni kuunga mkono za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania za kuhimiza matumizi ya nishati safi, uhifadhi wa mazingira na maendeleo endelevu.



Akizungumza katika Maonesho ya Kitaifa ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Malecela, Nzuguni jijini Dodoma, Daktari wa Mifugo kutoka Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Innocent Kimweri alisema kuwa seksheni ya mifugo kimebuni mfumo wa kuzalisha bayogesi kwa kutumia kinyesi cha mifugo na mabaki ya chakula. Alisema kuwa ubunifu huo unalenga kupunguza uchafuzi wa mazingira, kuboresha usimamizi wa taka na kuongeza matumizi ya nishati mbadala.

Akifafanua zaidi, alisema kuwa mfumo huo unahusisha kuchakata kinyesi cha mifugo na mabaki ya chakula kwa kuyapeleka kwenye mtambo maalumu unaozalisha bayogesi. Aliongeza kuwa nishati hiyo hutumika kwa shughuli mbalimbali ikiwemo kupikia, wakati joto linalozalishwa likitumika kuwahifadhi na kuwapa joto wanyama wadogo wanaozaliwa. Aidha, teknolojia hiyo husaidia kupunguza harufu mbaya, uchafuzi wa mazingira na gharama za matumizi ya nishati.

Dkt. Kimweri aliwahimiza wananchi, kujifunza na kutumia teknolojia hiyo katika maeneo yao ili kuboresha usimamizi wa taka, kulinda mazingira, kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza matumizi ya nishati safi. Aliongeza kuwa matumizi ya bayogesi pia yanasaidia kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, hatua inayochangia katika uhifadhi wa misitu na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Halmashauri ya Jiji la Dodoma inaendelea kutoa elimu na kuonesha teknolojia mbalimbali za kisasa katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi kupitia banda lake katika Maonesho ya Kitaifa ya Nanenane, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhamasisha matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira na kuongeza tija katika uzalishaji.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Barabara za Mtaa wa Mbwanga yafunguliwa, Diwani Kerenge aitaja kuwa chachu ya maendeleo

Kanda Namba Tatu yaimarisha ushirikiano na wamiliki wa vituo vya malezi ya watoto Dodoma

BANDA YA JIJI LA DODOMA LATOA TEKNOLOJIA UFUGAJI SAMAKI NA KUKU PAMOJA