AI Ultrasound kuokoa maisha ya Mama na Mtoto Dodoma
Na. Lulu Luvanda, MKONZE
Mkoa wa Dodoma umechaguliwa kuwa mkoa wa majaribio
katika matumizi ya teknolojia ya AI Ultrasound, kupitia Mradi wa The Study of
AI-Facilitated Ultrasound Feasibility and Assessment of Resources and
Integration (SAFARI Project), unaolenga kuboresha huduma za afya ya mama na
mtoto.
Hatua hiyo imekuja wakati wa hafla ya kukabidhi vifaa vya AI Ultrasound kwa vituo 32 vya kutolea huduma za afya katika Mkoa wa Dodoma, iliyofanyika katika Kituo cha Afya Mkonze, jijini Dodoma.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,
Rosemary Senyamule, alikipongeza Chuo
Kikuu cha Dodoma (UDOM) kwa kuendelea kufanya tafiti zenye uhalisia na
zinazolenga kutatua changamoto mbalimbali katika jamii, ikiwemo tafiti katika
sekta za Utalii, Mazingira pamoja na Lishe.
Alisema kuwa matumizi ya vifaa hivyo katika vituo vya
afya yatawezesha wananchi kupata huduma za awali kwa ukaribu zaidi, hivyo
kupunguza changamoto ya kusafiri umbali mrefu kutafuta huduma za uchunguzi wa Ultrasound.
Alishukuru kwa Dodoma kuchaguliwa kuwa mkoa wa majaribio wa matumizi ya teknolojia hiyo, akieleza kuwa uzoefu utakaopatikana unaweza kuwa msingi wa matumizi ya teknolojia hiyo katika mikoa mingine nchini Tanzania.
Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dkt. Thomas Ruta alisema kuwa AI Ultrasound
ni teknolojia yenye uwezo wa kusaidia katika uchunguzi wa mapema na hivyo
kuchangia katika kuokoa maisha ya mama na mtoto, hasa watoto wadogo.
Alisisitiza kuwa vifaa hivyo vinapaswa kutumika
ipasavyo na wataalamu wa afya, badala ya kuhifadhiwa stoo, huku akihimiza
maafisa afya na wauguzi kutumia teknolojia hiyo katika kutoa huduma bora, za
karibu na zenye utu kwa wananchi.
Comments
Post a Comment