Wananchi kupatiwa elimu ya fursa za kiuchumi na mikopo ya 7%

Na. Mwandishi wetu, DODOMA

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu fursa mbalimbali za kiuchumi na mikopo inayotolewa kupitia mifuko ya uwezeshaji wananchi kiuchumi, ikiwa ni sehemu ya shughuli za Mwezi wa Maendeleo ya Jamii, unaolenga kuwawezesha wananchi kujikwamua kiuchumi na kupunguza umaskini.



Akizungumza kuhusu shughuli za uwezeshaji zinazotekelezwa katika kipindi hicho, Mratibu wa Dawati la Uwezeshaji na Kupunguza Umaskini, Hidaya Mizega alisema kuwa wananchi wanaendelea kupewa elimu kuhusu fursa mbalimbali za kiuchumi, namna ya kuzifikia na kuzitumia kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao.

“Elimu hiyo pia inalenga kuwafahamisha wananchi kuhusu mikopo inayotolewa na halmashauri, ikiwemo mikopo yenye riba ya asilimia saba kwa wafanyabiashara wadogo maarufu kama machinga, ili kuwawezesha kukuza biashara zao na kuongeza kipato,” alisema Mizega.

Aliongeza kuwa wananchi wanapaswa kutumia fursa hizo kwa maendeleo yao, huku akisisitiza umuhimu wa kupata elimu sahihi kuhusu taratibu na namna ya kunufaika na fursa zinazotolewa kupitia mifuko mbalimbali ya uwezeshaji.

Halmashauri itaendelea kuwaunganisha wananchi na fursa mbalimbali za kiuchumi ili kuwasaidia kujenga uwezo wa kujitegemea, kuongeza kipato na kuchangia katika kupunguza umaskini katika jamii.

Comments

Popular Posts

Kata ya Miyuji Yaongeza Kasi ya Usimamizi Wa Usafi wa Mazingira

Kata za Nkuhungu na Kizota zajiandaa kukabiliana na mvua za El Nino

Mwenyekiti Mtaa wa Karume, Kata ya Mnadani ahamasisha usafi