Jiji la Dodoma laimarisha huduma za Kilimo na Mifugo

Na. Mwandishi wetu, DODOMA

 

Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma wamepokea taarifa ya utekelezaji wa shughuli za kilimo na mifugo kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026, ikiwemo utoaji wa chanjo, utambuzi na usajili wa mifugo, ukaguzi wa nyama na ‘Agrovet’, pamoja na udhibiti wa visumbufu vya mazao.

 

Akizungumza katika Mkutano wa Mwaka wa Baraza la Madiwani, Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Vincent Odero, alisema kuwa katika Mwaka wa Fedha 2024/2025 na 2025/2026, halmashauri ilitekeleza shughuli mbalimbali za kilimo na mifugo kwa lengo la kuongeza uzalishaji, kuimarisha usalama wa chakula na kuboresha huduma kwa wananchi.

 

Alisema kuwa shughuli hizo zilihusisha utoaji wa chanjo kwa mifugo, utambuzi na usajili wa mifugo kwa kutumia hereni za kielektroniki, uhamasishaji wa msimu wa kilimo pamoja na udhibiti wa wadudu na magonjwa katika mazao ya bustani na zabibu.

 

“Katika kipindi hiki, tumetekeleza shughuli mbalimbali za kilimo na mifugo kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kuongeza uzalishaji. Hali ya chakula imeimarika kutoka wastani mwaka 2024/2025 hadi kufikia kiwango kizuri Mwaka 2025/2026. Aidha, tumetambua na kusajili ng’ombe 15,177, mbuzi 5,618 na kondoo 1,015 kwa kutumia hereni za kielektroniki,” alisema Odero.

 

Odero aliongeza kuwa ukaguzi wa nyama umeongezeka, ambapo katika Mwaka 2024/2025 ng’ombe 46,876, mbuzi 63,267, kondoo 3,546 na kuku 376,213 walikaguliwa, idadi iliyoongezeka katika Mwaka 2025/2026 hadi kufikia ng’ombe 56,517, mbuzi 67,445, kondoo 3,919 na kuku 415,865, huku ukaguzi wa maduka ya dawa na pembejeo za mifugo (Agrovet) ukiongezeka kutoka 42 Mwaka 2024/2025 hadi 57 mwaka 2025/2026.

 

Akichangia taarifa hiyo, Diwani wa Kata ya Matumbulu, Godfrey Mtizi aliipongeza halmashauri hiyo kwa hatua inazoendelea kuchukua katika kuimarisha kilimo na ufugaji, akisema wananchi wanahitaji kuendelea kuona matokeo ya uwekezaji katika sekta hizo.

 

Alisema kuwa Kata ya Matumbulu ina wakulima na wafugaji, huku zabibu, mtama na mahindi kiwa miongoni mwa mazao muhimu ya biashara yanayolimwa katika eneo hilo, ambapo matarajio ya wananchi wanategemea huduma bora na maendeleo zaidi kutoka katika Jiji la Dodoma.

 

“Niipongeze Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kazi kubwa wanayoendelea kuifanya. Tunaamini katika bajeti ya Mwaka 2026/2027 wakulima na wafugaji wataendelea kukumbukwa katika kila sekta. Madiwani tutaendelea kutoa ushirikiano kwa halmashauri ili kutimiza matarajio ya wananchi wanayotarajia,” alisema Mtizi.

 

Utekelezaji wa shughuli hizo unaendelea kuimarisha sekta za kilimo na mifugo katika Jiji la Dodoma, huku ukilenga kuongeza uzalishaji, kuimarisha usalama wa chakula na kuboresha maisha ya wananchi, ambao wanaendelea kutarajia huduma na matokeo zaidi kutoka kwa halmashauri.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Kata ya Miyuji Yaongeza Kasi ya Usimamizi Wa Usafi wa Mazingira

Kata za Nkuhungu na Kizota zajiandaa kukabiliana na mvua za El Nino

Mwenyekiti Mtaa wa Karume, Kata ya Mnadani ahamasisha usafi