Maadhimisho ya Mwezi wa Maendeleo ya Jamii kutilia mkazo usafi Dodoma
Na. Lulu Luvanda, DODOMA
Halmashauri
ya Jiji la Dodoma imeandaa kampeni ya kuhamasisha wananchi kuhusu umuhimu wa
usafi katika Maadhimisho ya Mwezi wa Maendeleo ya Jamii yanayofanyika jijini
Dodoma Mwezi Septemba, 2026 kwa lengo la kuimarisha ushiriki wa jamii katika
kutunza mazingira.
Akizungumza
kuhusu maandalizi ya maadhimisho hayo Mkuu wa Divisheni ya Maendeleo ya Jamii
wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma Charity Sichouna, alisema kuwa wananchi watapewa elimu ya namna ya kuchangia
katika utunzaji wa mazingira bora kupitia tabia sahihi za kila siku.
Alisema
kuwa moja ya maeneo yatakayopewa kipaumbele ni usimamizi wa taka ngumu, ambapo
wananchi wataelimishwa kuhusu namna ya kuzihifadhi na kuzitenganisha kulingana
na aina zake kuanzia zinapozalishwa.
Kwa
mujibu wa Sichona kutenganisha taka katika chanzo kutarahisisha ukusanyaji na
uendeshaji wa taka, huku taka zinazoweza kutumika tena zikipata nafasi ya
kurejelewa badala ya kuishia katika maeneo yasiyokusudiwa.
Alisema
kuwa juhudi hizo zitaenda sambamba na kauli mbiu “Usafi ni Wajibu”, inayowataka
wananchi kutambua nafasi yao katika kuhakikisha maeneo wanayoishi na kufanyia
shughuli yanakuwa katika hali inayofaa.
Alisema
kuwa maadhimisho hayo yatahusisha kliniki ya shughuli za maendeleo, ambapo
wananchi watapata huduma na elimu kupitia madawati sita ya maendeleo, huku halmashauri
ikishirikiana na wadau mbalimbali, ikiwemo UN-Habitat, kuhamasisha ushiriki wa
jamii.
Aisha
aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika shughuli za maadhimisho hayo na
kutumia elimu watakayopewa kubadili tabia, ikiwemo kuhifadhi taka kwa usahihi
na kushiriki katika shughuli zinazolenga kuboresha mazingira na maendeleo ya
Jiji la Dodoma.
Comments
Post a Comment