Wafanyabiashara Soko la Miembeni Waazimia Kulinda Usafi

Na. Mohammed Ramadhani, DODOMA

Wafanyabiashara wa Soko la Miembeni jijini Dodoma wameahidi kuendelea kuimarisha usafi wa mazingira katika maeneo yao ya biashara, wakieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kulinda afya na ustawi wa jamii.



Akizungumza na waandishi wa habari, Katibu wa Soko la Miembeni, Adelgot Mbwani alisema kuwa uongozi wa soko unaendelea kuwahamasisha wafanyabiashara kufanya usafi mara kwa mara na kuhakikisha kila mmoja anawajibika kutunza mazingira yanayomzunguka katika eneo lake la biashara.

Aliongeza kuwa juhudi hizo pia zinaendana na msisitizo wa serikali wa kuhakikisha miji na maeneo ya biashara yanakuwa safi, hivyo wafanyabiashara wataendelea kushiriki kikamilifu katika kampeni za usafi. “Tumekuwa tukiwahamasisha wafanyabiashara wetu kufanya usafi mara kwa mara na kuwasisitizia kuwa usafi ni jukumu lao katika maeneo yao ya kazi, kama ambavyo Mheshimiwa Rais anavyosisitiza kuwa majiji yote yawe safi,” alisema Mbwani.

Kwa upande wake, Katibu wa Soko la Wauza Chuma, Benson Kihade alisema kuwa kampeni ya usafi imeanza katika Kanda Namba Moja ikiwa na lengo la kuhakikisha mazingira ya maeneo yote yanakuwa safi na salama.

Alisisitiza kuwa zoezi hilo linahusisha kata zote tisa zilizopo katika Kanda Namba Moja huku viongozi wa mitaa na kata, wenyeviti pamoja na wananchi wakishirikiana katika utekelezaji wa usafi wa mazingira.

Kihade alisema kuwa usafi huo hautakuwa wa muda mfupi, bali ni zoezi endelevu la kila siku litakalosimamiwa na viongozi pamoja na wananchi ili kuhakikisha mazingira yanabaki safi. “Sisi Kanda Namba Moja ambayo ipo katikati ya mji, kuanzia sasa tumeanza kampeni ya usafi wa kila siku katika kata zote tisa chini ya usimamizi wa watendaji wa mitaa, kata, wenyeviti na viongozi wengine wote. Tumeshirikiana na wananchi kufanya usafi wa mazingira zoezi ambalo litakuwa endelevu kwasababu tunajua maisha ya mwanadamu ni usafi” alisema.

Aidha, Kihade alitoa tahadhari kuwa hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wafanyaniashara watakaokiuka taratibu za usafi kwa kutotunza mazingira yao, akieleza kuwa kuwepo kwa adhabu kutasaidia kuongeza uwajibikaji miongoni mwa wafanyabiashara na wananchi.

Juhudi hizo zinaendelea kuhamasisha wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla kutambua kuwa usafi wa masoko na maeneo ya biashara ni sehemu muhimu ya kulinda afya ya jamii, kuboresha mazingira ya biashara na kuunga mkono azma ya kuwa na miji safi na salama.

 






Comments

Popular Posts

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lapitisha taarifa ya ufungaji hesabu 2025/2026

Wilaya ya Dodoma kuchanja watoto zaidi ya laki 2 chanjo ya Polio

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lampongeza Ndejembi kuteuliwa Makamu wa Rais