Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lampongeza Ndejembi kuteuliwa Makamu wa Rais

Na. Coletha Charles, DODOMA

 

Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Dodoma limempongeza Waziri wa Nishati na Mbunge wa Jimbo la Chamwino, Deogratius Ndejembi kwa kuteuliwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) tarehe 26 Agosti 2026.

 


Pongezi hizo zilitolewa na Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Bakari Fundikira wakati akiongoza Baraza maalum la Madiwani kwa ajili ya kupokea taarifa ya ufungaji wa hesabu za Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa mwaka ulioishia tarehe 30 Juni, 2026 katika ukumbi wa mikutano wa halmashauri hiyo.

 

Fundikira alisema kuwa Baraza zima la Madiwani linampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumuamini na kumteua Deogratius Ndejembi kushika nafasi hiyo ya Makamu wa Rais, huku akimtakiwa heri katika utekelezaji wa majukumu yake mapya.

 

“Lakini pia tutumie nafasi hii kumpongeza Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uteuzi alioufanya wa kumteua ndugu yetu Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, Baraza zima la Madiwani linampongeza sana,” alisema Fundikira.

 


Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Zuzu, Jenesta Malingo alisema kuwa uteuzi wa Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais ni hatua muhimu inayopaswa kupongezwa, akieleza kuwa nafasi hiyo inaonesha imani aliyopewa na Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuendelea kulitumikia taifa.

 

“Uteuzi wa mheshimiwa Ndejembi kuwa Makamu wa Rais ni jambo kubwa na la kujivunia. Tunampongeza Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumuamini na kumpa nafasi hii, na tunamtakia mheshimiwa Ndejembi kila la heri katika majukumu yake mapya ya kulitumikia taifa,” alisema Malingo.

 


Uteuzi huo ulitangazwa na Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Asha-Rose Migiro, Agosti 26, 2026 katika Ofisi Ndogo za CCM, Lumumba, Dar es Salaam, baada ya Ndejembi kupendekezwa kuchukua nafasi ya Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi aliyejiuzulu. Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilimthibitisha Agosti 28, 2026 kwa kura 324 sawa na asilimia 100 huku hatua inayofuata ikiwa ni kuapishwa rasmi kabla ya kuanza majukumu yake mapya ya Umakamu wa Rais.

Comments

Popular Posts

Vijana watakiwa kujiendeleza nje ya mfumo rasmi

NGOs zatakiwa kuzingatia uwazi na uwajibikaji Dodoma

Uendelevu wa NGOs wapatiwa msukumo wilayani Dodoma