Wilaya ya Dodoma kuchanja watoto zaidi ya laki 2 chanjo ya Polio
Na. Coletha Charles, NKUHUNGU
Wilaya ya Dodoma
imejipanga kuchanja watoto 207,096 chini ya miaka 10
dhidi ya ugonjwa wa Polio, sawa na asilimia 21 ya lengo la mkoa mzima, ikiwa ni
utekelezaji wa kampeni ya kitaifa ya kujikinga na mlipuko wa ugonjwa huo.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo, iliyofanyika katika Shule ya Msingi Nkuhungu, Kata ya Nkuhungu Halmshauri ya Jiji la Dodoma Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri alisema kuwa wilaya hiyo imekamilisha maandalizi yote ya kimkakati kupitia vikao vya ngazi tatu wataalamu, makundi ya hamasa na Kamati ya Afya ya Msingi ya Wilaya.
“Waliopewa
kazi ya kuhamasisha, wafanye kazi hiyo ya uhamasishaji kikamilifu. Na kwa
bahati njema, kama ambavyo tumeona hapa, wanatoka kwenye ngazi ya jamii, kwa
hiyo wanafahamu namna ya kushirikiana na jamii. Tumepewa lengo la kuchanja watoto
207,096,” alisema Alhaj Shekimweri.
Alitumia
nafasi hiyo kubainisha kuwa nchi haina mgonjwa wa Polio kwa sasa, hatua hiyo ni
maelekezo ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuendelea kulinda afya za
watoto. Aidha, alisisitiza kuwa zoezi hilo
linapaswa kufanyika kwa ufanisi ili kuhakikisha hakuna dosari.
Kwa
upande wake, Mwalimu Mkuu Msaidizi wa Shule ya Msingi Nkuhungu, Mwl. Rogathe Makupa
alisema kuwa zoezi la chanjo shuleni hapo limekwenda vizuri, ambapo kati ya
wanafunzi 2,957, wanafunzi 1,360 ni walengwa wamepatiwa chanjo ya Polio.
“Niwaase wazazi ambao bado watoto wao hawajaweza kupatiwa chanjo, waweze kuwaleta watoto ili waweze kupatiwa chanjo hii ya Polio. Lakini pia kuna wauguzi wanapita mtaani kwa ajili ya zoezi hili zima la chanjo. Kwa hiyo tunaomba
tushirikiane
nao katika zoezi zima la kufanikisha utoaji wa chanjo ya Polio,” alisema Mwl.
Makupa.
Naye,
Diwani wa Kata ya Nkuhungu, Julius Machea alisema kuwa anampongeza Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa chanjo hizo
ili kuwalinda watoto wa taifa la kesho.
“Kwangu
mimi, niendelee tu kusititiza wananchi wote, wahudumu, walezi, wazazi, tuendelee
kuleta watoto ili waweze kupata chanjo. Watu wote waone umuhimu wa jambo hili
kwa uzito," alisema Machea.
Hata
hivyo, Mkazi wa Nkuhungu Halmshauri ya Jiji la Dodoma, Rosemary Joseph
aliwasihi wazazi ambao bado hawajawapeleka watoto wao kupata chanjo kufanya
hivyo, akisisitiza kuwa chanjo ni muhimu katika kuwalinda watoto dhidi ya
magonjwa.
“Nawashauri wazazi wenzangu wawapeleke
watoto kupata chanjo ili ziweze kuwalinda watoto wetu. Pia ninamshukuru Mungu kwa kutuwezesha
kupata chanjo. Pia naishukuru serikali na Mama Samia kwa kuhakikisha chanjo
zinawafikia watoto wetu. Kwa kweli nimefurahi kwa sababu nilipomleta mtoto
wangu mwingine shuleni, nilielezwa kuwa mtoto huyu pia anaweza kupata chanjo
hapa,” alisema Joseph.
Kwa ujumla, serikali imewataka wazazi na
walezi katika Wilaya ya Dodoma kutumia fursa hiyo kuhakikisha watoto walio
chini ya miaka 10 wanapata chanjo ya Polio, huku ikisisitiza kuwa ushirikiano
wa jamii, viongozi na wahudumu wa afya ni muhimu katika kufanikisha kampeni
hiyo na kuzuia kurejea kwa ugonjwa huo nchini.
MWISHO
Comments
Post a Comment