RC Kheri James: Elimu iwe silaha yenu dhidi ya rushwa

Na. Muhamad  Said, IRINGA

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James amewataka wanafunzi wa klabu za wapinga rushwa kutoka mikoa ya Iringa na Dodoma kuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya rushwa, akisisitiza kuwa elimu na uadilifu ni msingi muhimu wa kujenga taifa lenye maendeleo endelevu.


Akizungumza katika mdahalo wa klabu za wapinga rushwa za shule za msingi na sekondari unaofanyika katika Ukumbi wa Shule ya Sekondari Lugalo, amewahimiza wanafunzi kutambua madhara ya rushwa na kuanza mapema kujenga utamaduni wa kuikataa, akieleza kuwa kizazi cha leo ndicho kitakachobeba dhamana ya uongozi na maendeleo ya taifa hapo baadaye.

 

Alisisitiza kuwa suala la kupinga rushwa linapaswa kupigwa vita na watu wote wakiwemo wanafunzi, akiongeza kuwa vijana wanapaswa kuwa mabalozi wa uadilifu katika shule zao, familia na jamii kwa ujumla kwa kukataa vitendo vya rushwa na kuhamasisha wenzao kusimamia haki na uwajibikaji.

 

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka wanafunzi kutumia midahalo kama fursa ya kujenga maarifa, kujiamini na kubadilishana mawazo, badala ya kuiona kama uwanja wa kushindana kwa namna inayoweza kuwagawa akisema kuwa ushindani unaofaa katika midahalo ni ule unaojenga uwezo wa kufikiri, kujenga hoja na kujifunza kutoka kwa wengine.

 


“Msishindane kwa lengo la kumshinda mwenzenu tu, shindaneni kwa lengo la kujifunza, kubadilishana maarifa na kujenga uwezo wa kufikiri. Mshindi wa kweli ni yule anayepata maarifa zaidi” alisema Kheri.

 

Alihitimisha kwa kusema kuwa taifa linahitaji kizazi cha vijana wenye maarifa na misingi imara ya maadili ambao watakapokuwa viongozi, wataalamu na watendaji katika sekta mbalimbali watasimamia rasilimali za nchi kwa uaminifu na kuweka mbele maslahi ya watanzania. 


Comments

Popular Posts

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lapitisha taarifa ya ufungaji hesabu 2025/2026

Wilaya ya Dodoma kuchanja watoto zaidi ya laki 2 chanjo ya Polio

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lampongeza Ndejembi kuteuliwa Makamu wa Rais