LAAC yalipongeza Jiji la Dodoma kwa ubunifu wa Jengo Jumuishi Kituo cha Afya Makole

Na. Mwandishi Wetu, VIWANDANI

 

Halmshauri ya Jiji la Dodoma imepongezwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kwa ubunifu wa kujenga jengo jumuishi la huduma za afya la ghorofa tatu katika Kituo cha Afya Makole lenye gharama ya shilingi bilioni 6.9 hatua inayolenga kutatua changamoto ya uhaba wa eneo na kukidhi ongezeko la mahitaji ya huduma za afya katika jiji hilo.

 


Pongezi hizo zilitolewa na Makamu Mwenyekiti wa (LAAC), Abdallah Chikota wakati wa ziara ya kamati hiyo ya kukagua miradi ya maendeleo Kata ya Viwandani Jiji la Dodoma.

 

Chikota alisema kuwa mfumo wa kujenga ghorofa ulikuwa ndio mbadala sahihi wa kukabiliana na changamoto ya uhaba wa eneo na kupanua huduma za matibabu, bila kulazimika kutafuta eneo jipya nje ya kituo hicho cha afya.

 

“Kwanza tunalipongeza Jiji la Dodoma kwa ubunifu wao na mawazo ya kisasa kwa sababu hapa Kituo cha Afya Makole kuna changamoto ya eneo, kwa hiyo ili kutatua tatizo hilo wameamua kujenga jengo la ghorofa tatu. Jengo hili likikamilika tutakuwa na kituo cha hadhi ya juu katika jiji letu la Dodoma,” alisema Chikota.

 




Aliongeza kuwa ubunifu huo ni muhimu zaidi kutokana na ongezeko kubwa la mahitaji ya huduma za afya katika Jiji la Dodoma, akibainisha kuwa kukamilika kwa mradi huo kutaifanya Makole kuwa na uwezo wa kutoa huduma kwa hadhi ya hospitali ya jiji.

 

Akisoma taarifa hiyo, Kaimu Mkurugenzi wa Jiji, Vincent Odero, alisema kuwa mradi huo umechangiwa na uwekezaji unaohitajika kutokana na ongezeko la idadi ya watu na mahitaji ya huduma za afya katika Kituo cha Afya Makole, kilichopo katikati ya jiji.

 


Aliongeza kuwa takwimu zinaonesha kuwa idadi ya wanawake waliojifungua kwa njia ya kawaida iliongezeka kutoka 3,683 mwaka 2017 hadi 6,989 mwaka 2025, huku waliojifungua kwa njia ya upasuaji ikiongezeka kutoka 226 hadi 957 katika kipindi hicho.

 

Kwa ujumla, LAAC imeridhishwa na utekelezaji wa mradi huo wa jengo jumuishi la huduma za afya katika Kituo cha Afya Makole, unaotekelezwa kwa ushirikiano wa fedha kutoka serikali kuu pamoja na mapato ya ndani ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Comments

Popular Posts

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lapitisha taarifa ya ufungaji hesabu 2025/2026

Wilaya ya Dodoma kuchanja watoto zaidi ya laki 2 chanjo ya Polio

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lampongeza Ndejembi kuteuliwa Makamu wa Rais