Wananchi watakiwa kufanya usafi kila siku kuweka Dodoma safi

Na. Leah Mabalwe, DODOMA

Wananchi na wafanyabiashara katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma wametakiwa kufanya usafi kila siku katika maeneo yao badala ya kusubiri siku ya jumamosi ya mwisho wa wiki ili kuhakikisha mazingira yanakuwa safi, salama na rafiki kwa afya za jamii.



Wito huo ulitolewa na Meneja Kanda Namba Moja, Nicholaus Mitembo mara baada ya kushiriki zoezi la usafi wa pamoja katika Soko la Miembeni Jijini Dodoma, ambapo amesisitiza kuwa usafi si jukumu la mamlaka pekee bali ni wajibu wa kila mwananchi na mfanyabiashara.

 

Alisema kuwa msisitizo huo unatokana na kauli iliyotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule katika kikao na Maafisa Mazingira pamoja na maafisa afya ambapo alisisitiza kuwa kufanya usafi siku ya Jumamosi pekee haitoshi. “Usafi wa Jumamosi pekee hautoshi. Kila mwananchi na mfanyabiashara ana wajibu wa kushiriki katika usafi kila siku. Niwasihi wananchi wote pamoja na wafanyabiashara tusisubiri siku ya Jumamosi pekee, bali tuwe tunafanya usafi kila siku katika maeneo yetu ili kuhakikisha tunakuwa na mazingira safi na salama,” alisema Mitembo.

 

Kwa upande wake, mfanyabiashara wa Soko la Miembeni, Saida Shabani alisema kuwa wana wajibu wa kuhakikisha maeneo ya biashara zao yanakuwa safi wakati wote kwasababu mazingira safi ni sehemu muhimu ya kuwavutia wateja. “Tumefanya usafi katika eneo letu hapa Korongoni, sokoni lakini naomba nitoe wito kwa wafanyabiashara wenzangu tufanye usafi kila siku. Haya ndiyo maeneo yetu ya kazi, hivyo tukiyaacha yakiwa machafu na mazingira yakiwa mabovu, wateja hawatafika. Tujitahidi kufanya usafi kila siku katika maeneo yetu ya kazi pamoja na maeneo yetu ya nyumbani” alisema Shabani.

 

Ushirikiano wa wananchi, wafanyabiashara na wadau mbalimbali katika kuzingatia usafi wa mazingira unatarajiwa kuendelea kuwa msingi wa kulifanya Jiji la Dodoma kuwa safi, salama na lenye mazingira bora kwa wakazi, wafanyabiashara na wageni.





Comments

Popular Posts

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lapitisha taarifa ya ufungaji hesabu 2025/2026

Wilaya ya Dodoma kuchanja watoto zaidi ya laki 2 chanjo ya Polio

Wafanyabiashara Soko la Miembeni Waazimia Kulinda Usafi