Vijana Dodoma na Iringa Kukutana Kupaza Sauti Dhidi ya Rushwa

Na. Muhamad Said, IRINGA

Wanafunzi kutoka klabu za wapinga rushwa za shule za msingi na sekondari za mikoa ya Dodoma na Iringa leo wanatarajiwa kukutana katika mdahalo maalumu wa mapambano dhidi ya rushwa.



Mdahalo huo utafanyika katika Ukumbi wa Shule ya Sekondari Lugalo, mkoani Iringa, ukilenga kuwajengea wanafunzi uelewa, kuimarisha maadili na kuongeza ushiriki wa vijana katika mapambano dhidi ya rushwa ndani ya shule na jamii kwa ujumla.

Kupitia mdahalo huo, wanafunzi wanatarajiwa kutoa hoja kuhusu madhara ya rushwa kwa jamii na taifa pamoja na changamoto zinazoweza kujitokeza katika mapambano dhidi ya vitendo hivyo. Aidha, mjadala unatarajiwa kutoa nafasi kwa vijana kueleza namna wanavyoweza kuwa sehemu ya mabadiliko katika kujenga jamii inayozingatia uadilifu.

Ushirikishwaji wa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari unatarajiwa pia kuifanya shughuli hiyo kuwa sehemu ya kuwaandaa vijana kuwa mabalozi wa maadili na mapambano dhidi ya rushwa, kwa kuanza kujenga uelewa na msimamo wao tangu wakiwa katika hatua za awali za elimu.

Mdahalo huo unatarajiwa kuangazia pia umuhimu wa klabu za wapinga rushwa shuleni katika kutoa elimu kwa wanafunzi, kuhamasisha uadilifu na kuwapa vijana nafasi ya kujadili masuala yanayogusa maendeleo ya jamii.

 

Comments

Popular Posts

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lapitisha taarifa ya ufungaji hesabu 2025/2026

Wilaya ya Dodoma kuchanja watoto zaidi ya laki 2 chanjo ya Polio

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lampongeza Ndejembi kuteuliwa Makamu wa Rais