RC Dodoma amtaka Mkandarasi kuongeza kasi ukarabati Soko la Majengo
Na. Mohammed Ramadhani, MAJENGO
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule amemtaka
mkandarasi anayetekeleza ukarabati wa Soko la Majengo jijini Dodoma kuongeza
kasi ya kazi ili kukamilisha mradi huo ndani ya muda wa nyongeza wa siku 60
uliotolewa.
Senyamule alitoa kauli hiyo wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya ukarabati wa Soko la Majengo, akieleza kuwa soko hilo lina mchango mkubwa katika kutoa huduma na kukidhi mahitaji ya wananchi wa Jiji la Dodoma.
Akizungumza baada ya kukagua maendeleo ya mradi huo,
mkuu huyo wa mkoa alisema kuwa utekelezaji wa kazi unaelekea vizuri, lakini
mkandarasi anapaswa kutumia kikamilifu muda wa nyongeza aliopewa ili
kuhakikisha kazi zilizobaki zinakamilika kwa wakati.
Aidha, alishauri kuwa mkandarasi kuongeza muda wa
utekelezaji wa kazi kwa kufanya kazi hadi nyakati za usiku kwa kutumia taa,
akisema hatua hiyo itasaidia kuongeza kasi ya ujenzi na kuhakikisha mradi
unakamilika kwa wakati.
Alisisitiza umuhimu wa kukamilisha kazi kabla ya kuanza kwa mvua, akieleza kuwa kuchelewa kwa utekelezaji kunaweza kuathiri kasi ya mradi na kuongeza changamoto katika kipindi cha mvua.
Soko la Majengo linatarajiwa kuwa sehemu muhimu katika
utoaji wa huduma na mahitaji mbalimbali kwa wananchi wa Jiji la Dodoma, huku serikali
ikiendelea kusimamia utekelezaji wa mradi huo ili ukamilike kwa wakati na
kuanza kutoa huduma iliyokusudiwa.
Comments
Post a Comment