Teknolojia ya Kinengunengu mkombozi kwa vifaranga vya kuku Dodoma

 Na. Mwandishi wetu, NZUGUNI

Halmashauri ya Jiji la Dodoma limeibua ubunifu mpya wa teknolojia ya banda maalumu la kufugia vifaranga vya kuku maarufu kama ‘Kinengunengu’ linalolenga kuwasaidia wafugaji kupata njia bora ya kuwapatia vifaranga joto, chakula, malazi na mazingira salama ya ukuaji.



Banda hilo limekuwa miongoni mwa vivutio vikubwa katika maonesho ya Nanenane yanayofanyika katika viwanja vya Dkt. John Malecela, Nzuguni kupitia banda la Jiji la Dodoma, ambapo wananchi wamekuwa wakijitokeza kwa wingi kujifunza namna ya kuanza na kuendeleza ufugaji wa kuku kwa njia rahisi na salama.

Akielezea banda hilo, Afisa Mifugo wa Jiji la Dodoma, Delila Mlamka alisema kuwa wafugaji wengi wamekuwa wakitegemea matumizi ya taa na mkaa kwa ajili ya kuwapatia vifaranga joto, lakini teknolojia ya Kinengunengu imekuja kuondoa utegemezi huo kwa kutumia muundo unaoweza kuhifadhi joto ndani ya banda.

Alisema kuwa Kinengunengu kimeundwa katika mfumo wenye sehemu mbili muhimu, sehemu ya kulala ambayo huzibwa zaidi wakati wa usiku ili kuhifadhi joto, na sehemu ya kula ambayo huwa wazi kwa juu na sehemu ya vifaranga hao kutumia mchana ili kuruhusu upatikanaji wa chakula na hewa ya kutosha.



“Jiji la Dodoma limeunda Kinengunengu ili kuwapa wafugaji elimu ya vitendo kuhusu namna ya kuhudumia vifaranga katika hatua za mwanzo. Banda hili linasaidia kuhakikisha vifaranga wanapata joto linalohitajika, chakula, maji safi na mazingira yanayowalinda dhidi ya changamoto mbalimbali,” alisema Mlamka.

Aliongeza kuwa teknolojia hiyo inalenga kuwasaidia wafugaji kupunguza gharama za uzalishaji, hasa gharama za kununua mkaa au kutumia umeme kwa ajili ya taa za joto, huku ikisaidia pia kupunguza changamoto za vifo vya vifaranga vinavyosababishwa na baridi.

Kwa upande wake mfugaji wa kuku kutoka Kata ya Nzuguni, jijini hapa, Prisca Chana alisema kuwa banda hilo limeonesha kuwa ufugaji wa kisasa unaweza kuanza kwa kutumia ubunifu unaopatikana ndani ya mazingira ya mfugaji.

“Kinachowafanya vifaranga wakue vizuri ni kupata mazingira sahihi. Teknolojia hii imesaidia kuonesha kuwa mfugaji anaweza kutunza joto bila kutegemea gharama kubwa za mkaa au taa,” alisema Chana.

Nae, mkazi wa Kata ya Nala, Julias Kesi anayetamani kuanza kufuga kuku lakini anaishi kwenye nyumba ya kupanga alisema kuwa ubunifu huo umempa matumaini ya kuanza ufugaji kwa kiwango kidogo.

“Changamoto yangu ilikuwa nafasi na gharama za kuendesha ufugaji, lakini baada ya kuona Kinengunengu nimegundua kuwa naweza kuanza na idadi ndogo ya vifaranga bila kutumia vifaa vya gharama kubwa,” alisema Kesi.

Ubunifu wa teknolojia ya Kinengunengu ni sehemu ya jitihada za kuhamasisha ufugaji bora wa kuku na kuwasaidia wananchi kuongeza kipato kupitia teknolojia rahisi, nafuu na inayozingatia mahitaji ya vifaranga.

Comments