Silage suluhisho la uhaba wa chakula cha ng'ombe Dodoma

Na. Mwandishi wetu, NZUGUNI

Wafugaji wa ng’ombe katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma wamehimizwa kuanza kutengeneza na kuhifadhi chakula cha mifugo kilichochachushwa (Silage) ili kuhakikisha mifugo inapata lishe ya kutosha wakati wa kiangazi, kipindi ambacho maeneo mengi hukumbwa na upungufu mkubwa wa malisho kutokana na ukame.



Rai hiyo ilitolewa na Afisa Mifugo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Delila Mlamka wakati akiwaelezea wananchi waliotembelea banda la mifugo la halmashauri hiyo katika maonesho ya Nanenane yanayoendelea jijini hapa.

Alisema kuwa Silage ni chakula kinachotengenezwa kwa kuchanganya majani mabichi yaliyokatwakatwa, kiasi kidogo cha majani makavu, pumba na molases, kisha kuhifadhiwa kwenye mazingira yasiyoruhusu hewa ya oksijeni kuingia kwa siku 21 ili kichachuke vizuri na kuwa salama kwa matumizi ya mifugo.

Alisema kuwa chakula hicho  kinaweza kutengenezwa kwenye mashimo au mapipa na kuhifadhiwa katika mifuko midogo ya plastiki na mifuko maalumu ya kuhifadhia nafaka ‘kinga njaa’, ila tu hewa isiingie ndani ya kifungashio.

“Silage ni lishe bora na kinapendwa sana na ng’ombe wa maziwa kwa sababu kina mchanganyiko wa majani, pumba na molases unaosaidia kuongeza virutubisho muhimu kwa ukuaji wa mifugo na uzalishaji wa maziwa. Chakula hiki kinaweza kuhifadhiwa kwa zaidi ya miaka miwili bila kuharibika endapo kitaandaliwa na kuhifadhiwa kwa usahihi,” alisema Mlamka.



Kwa upande wake mfugaji wa ng’ombe kutoka Kata ya Nzuguni, Mussa Elisha alisema kuwa teknolojia ya silage itakuwa msaada mkubwa kwa wafugaji, hasa wakati wa kiangazi ambapo malisho hupungua kwa kiasi kikubwa.

“Hapo zamani tulipata wakati mgumu kulisha mifugo kipindi cha ukame, lakini sasa tukitengeneza silage mapema tunakuwa na uhakika wa chakula kwa muda mrefu. Hii itachangia mifugo yetu kubaki na afya nzuri na uzalishaji wa maziwa kuendelea hata wakati wa kiangazi,” alisema Elisha.

Kwa upande wake mdau wa mifugo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Elineema Kikumbi alisema kuwa utunzaji wa malisho kupitia teknolojia ya silage ni hatua muhimu ya kuongeza tija katika sekta ya mifugo na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Dodoma ni moja ya maeneo yanayokumbwa na ukame mara kwa mara. Wafugaji wanapaswa kutumia kipindi cha mvua kuandaa akiba ya chakula cha mifugo. Silage ni suluhisho la kudumu ambalo litasaidia kupunguza vifo vya mifugo, kuongeza uzalishaji na kuinua kipato cha wafugaji,” alisema Kikumbi.

Wataalamu wa mifugo wanaendelea kuhimiza wafugaji kuwekeza katika utengenezaji wa silage ili kuwa na akiba ya malisho mwaka mzima, hatua itakayosaidia kuongeza uzalishaji wa maziwa na nyama pamoja na kuimarisha ustahimilivu wa sekta ya mifugo dhidi ya ukame.

 

Comments