Meya Chaula: Kanda za utoaji huduma kusogeza huduma kwa wananchi Dodoma

Na. Mwandishi wetu, MAKUTUPORA

Uanzishwaji wa kanda za utoaji huduma katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma ni mkakati unaolenga kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi, kuongeza ufanisi wa utendaji kazi na kuharakisha maendeleo katika maeneo yote ya jiji.


Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika jijini Dodoma, Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula  alisema kuwa mfumo wa kanda utarahisisha upatikanaji wa huduma mbalimbali za halmashauri, kupunguza muda wa wananchi kufuata huduma katika makao makuu ya jiji na kuongeza uwajibikaji kwa watendaji.

Chaula ambae ni Diwani wa Kata ya Makutupora alisema kuwa kata hiyo ipo katika Kanda Namba Sita hivyo,  wananchi watapata huduma kwa urahisi zaidi, zikiwemo huduma za usafi wa mazingira, ukusanyaji wa mapato, usimamizi wa miradi ya maendeleo, pamoja na kushughulikia changamoto zinazojitokeza katika maeneo yao kwa wakati.

“Madhumuni ya uanzishwaji wa kanda hizi ni kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma bora bila kulazimika kusafiri umbali mrefu. Tunataka kuimarisha ushirikiano kati ya viongozi na wananchi ili maendeleo yafike kwa kila mmoja,” alisema Chaula.

Aidha, aliwataka wananchi kushirikiana na viongozi wa kanda, kulinda miundombinu ya umma na kushiriki katika shughuli za maendeleo ili kufanikisha malengo ya kuboresha utoaji wa huduma ndani ya Jiji la Dodoma.



Kwa upande wake mkazi wa Kata ya Makutupora, Godfrey Kimario alisema kuwa kanda hizo zimewarahisishia wao kupata huduma kwasababu walikuwa wakilazimika kusafirisi  umbali mrefu hadi ofisi za jiji kufuata huduma mfano, kulipa tuu leseni na ushuru wa huduma lakini sasa ni rahisi kwasababu kanda ipo karibu nao.

“Tunaishukuru ofisi ya mkurugenzi kwa kusogeza huduma kupitia kanda maana sasa maafisa biashara wanapita katika mitaa yetu kwaajili ya kukusanya tozo mbalimbali tofauti na hapo awali ambapo tulilazimika kwenda hadi jiji” alisema Kimario

Mkutano huo ulihudhuriwa na viongozi wa serikali za mitaa, watendaji wa halmashauri, pamoja na wananchi wa Kata ya Makurupora ambapo walielezwa utekelezaji wa mfumo wa kanda utasaidia kupunguza msongamano wa wananchi wanaofuata huduma katika ofisi za makao makuu ya halmashauri na kuongeza kasi ya utatuzi wa kero za wananchi.





 

Comments

Popular Posts

Barabara za Mtaa wa Mbwanga yafunguliwa, Diwani Kerenge aitaja kuwa chachu ya maendeleo

Kanda Namba Tatu yaimarisha ushirikiano na wamiliki wa vituo vya malezi ya watoto Dodoma

BANDA YA JIJI LA DODOMA LATOA TEKNOLOJIA UFUGAJI SAMAKI NA KUKU PAMOJA