Jiji la Dodoma lawapa vijana fursa mikopo ya 10%

Na. Mwandishi wetu, DODOMA

HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imeendelea kuwawezesha vijana kiuchumi kupitia mikopo ya asilimia 10, hatua inayowapa nafasi ya kuanzisha na kuendeleza shughuli mbalimbali za uzalishaji, ikiwemo viwanda vidogo, utengenezaji wa bidhaa na utunzaji wa mazingira.



Hayo yalisemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’wale, Husna Toni mara baada ya kutembelea vikundi vya vijana vinavyofanya shughuli mbalimbali katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Alisema kuwa ziara hiyo imetoa fursa ya kujifunza namna vijana wa Jiji la Dodoma wanavyotumia mikopo ya asilimia 10 kujiajiri, kuongeza kipato na kuchangia maendeleo ya jamii. “Vijana wa Dodoma wana uthubutu mkubwa katika shughuli za uzalishaji, viwanda na utunzaji wa mazingira. Hii inatuonesha kwamba fursa zipo na vijana wakipewa mitaji na mazingira mazuri wanaweza kujiajiri na kuwa sehemu muhimu ya maendeleo ya taifa” alisema Toni.

Aliongeza kuwa vijana wanapaswa kutumia fursa zinazopatikana, hususan mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na serikali kupitia Mamlaka za Serikali za Mitaa, kwa kuanzisha shughuli zenye tija na zinazoweza kuwaongezea kipato.

Kwa upande wake Afisa Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale, Estellia Colman alisema kuwa utekelezaji wa mikopo hiyo umeendelea kuwafungua vijana macho na kuwafanya kuona kuwa wanaweza kujiajiri na kujenga maisha yao kupitia mitaji midogo wanayoipata. “Kupitia fursa hizi, tumejifunza kwamba kumbe vijana wanaweza kujiajiri na kuendesha shughuli za kiuchumi kupitia mikopo ya asilimia 10. Tunachohitaji ni vijana kuzitambua fursa hizi, kujiunga katika vikundi na kutumia mikopo kwa malengo yaliyokusudiwa” alisema Colman.



Ziara hiyo imeendelea kuonesha namna uwezeshaji wa vijana kupitia mikopo unavyoweza kuchochea ajira, ujasiriamali, uzalishaji viwandani, usafi wa mazingira na maendeleo ya kiuchumi katika jamii ambapo kikundi kinachojihusisha na utengenezaji wa viatu na kikundi kinachofanya shughuli za uzoaji taka vilitembelewa.

Comments

Popular Posts

Barabara za Mtaa wa Mbwanga yafunguliwa, Diwani Kerenge aitaja kuwa chachu ya maendeleo

Kanda Namba Tatu yaimarisha ushirikiano na wamiliki wa vituo vya malezi ya watoto Dodoma

BANDA YA JIJI LA DODOMA LATOA TEKNOLOJIA UFUGAJI SAMAKI NA KUKU PAMOJA