Jiji la Dodoma laibuka na zana za upaliliaji, Maonesho ya Nanenane

Na. Mwandishi wetu, DODOMA

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imeendelea kung’ara katika Maonesho ya Nanenane kwa kuweka vitu vya kitofauti kama zana za upaliliaji ambazo zimeundwa na mjasiriamali mdogo wa ndani ya jiji.




Akizungumza na waandishi wa habari mjasiriamali, Zuberi Nguzo aliyepata fursa ya kuonesha ujuzi katika maonesho hayo alisema kuwa zana hizo zimeundwa kwa muundo wa ‘power tiller’ ya miguu mitatu zikiwa katika ubora wa hali ya juu.

“Zana hizi za upaliliaji zinatumia injini ya guta lakini ina mfumo wa rejeta kama kawaida. Pia ina mfumo wa feni na upande wa nyuma kuna jembe ambalo hili ndilo linatumika kwa ajili ya upaliliaji. Katika upaliliaji inatumia mfumo wa matuta kwa maana kwamba inapita katikati ya mstari na kuweka matuta kwenye mashina ya mahindi kwasababu tairi zake tumeweka kwa kipimo cha sentimita 62, hiki ni kipimo sahihi kabisa kwa upana kwa kilimo cha mahindi,” alisema Nguzo.

Alisema kuwa ameamua kubuni zana hizo kwasababu baadhi ya vifaa vya kuundia vinapatikana kiurahisi mfano, kiti cha gari, injini ya guta na minyororo ya pikipiki, mambo ambayo yanamfanya kuunda zana zenye tija katika jamii.



Aliongeza kuwa katika maonesho ya Nanenane kuna vitu ambavyo mwananchi akitembelea katika banda la Jiji la Dodoma atajifunza mengi zaidi na kuweza kupata fursa ya kujikwamua kiuchumi.

Kwa upande wake Said Mohamed, mkazi wa Dodoma alisema kuwa amepata kujifunza mengi katika banda la Jiji la Dodoma, kikubwa kikiwa ni zana za upaliliaji ambazo zimeundwa kwa mkono na mjasiriamali wa Dodoma ambazo zinatumika kupapilia mahindi na zinapatikana kiurahisi.

“Maonesho haya ni fursa kwa wakazi wa Dodoma, nawashauri waje watembelee katika banda hili la jiji kwasababu watajifunza mengi kama matumizi ya zana za upaliliaji, kilimo cha mahindi, kilimo cha ngano na kabeji nyekundu ambayo ni nadra sana kuiona katika jamii. Lakini hapa nimeona na nimeelezwa faida zake,” alisema Mohamed.



Halmashauri ya Jiji la Dodoma inaendelea kuwakaribisha wananchi wote kutembelea mabanda yake likiwemo banda la mifugo na uvuvi ili kuweza kujifunza masuala mbalimbali.

 

Comments

Popular Posts

Barabara za Mtaa wa Mbwanga yafunguliwa, Diwani Kerenge aitaja kuwa chachu ya maendeleo

Kanda Namba Tatu yaimarisha ushirikiano na wamiliki wa vituo vya malezi ya watoto Dodoma

BANDA YA JIJI LA DODOMA LATOA TEKNOLOJIA UFUGAJI SAMAKI NA KUKU PAMOJA