Jiji la Dodoma kuwa kinara ushirikiano na TBS

Na. Mwandishi wetu, DODOMA

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imewataka maafisa afya na watumishi wa sekta mbalimbali kuimarisha ushirikiano na kutumia ipasavyo mafunzo ya matumizi ya mfumo wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ili kuongeza ufanisi katika ukaguzi na usajili wa bidhaa.



Akifungua mafunzo hayo, Mganga Mkuu wa Jiji la Dodoma, Dkt. Sebastian Pima alisema kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo washiriki kutumia mfumo wa TBS kwa usahihi ili shughuli zote za ukaguzi na usajili ziweze kufanyika kwa ufanisi kupitia mfumo huo.

“Kila mmoja anatakiwa kushirikiana na wenzake, hizi ni kazi za timu, si za mtu mmoja. Tunataka Dodoma iwe mfano wa kuigwa nchini katika utekelezaji wa majukumu ya ushirikiano kati ya TBS na halmashauri, kila afisa atapangiwa malengo ya kila siku na kila wiki yatakayosaidia kuongeza utendaji na kufikia malengo ya ukusanyaji wa mapato pamoja na kuboresha huduma kwa wananchi," alisema Dkt. Pima.

Aidha, aliwahimiza washiriki kutumia fursa ya uwepo wa wataalamu wa TBS kuuliza maswali na kutatua changamoto zote zinazohusu matumizi ya mfumo, akisisitiza kuwa ushirikiano na kujituma ndiyo msingi wa mafanikio.



Kwa upande wake Afisa Mwandamizi wa TBS Kanda ya Kati, Donisian Lutahala alisema kuwa mafunzo hayo yalilenga kuongeza uelewa wa wakaguzi kuhusu namna bora ya kutekeleza majukumu yao ili kuongeza ufanisi na matokeo chanya katika kazi.

“Mafunzo haya yana umuhimu mkubwa kwa sababu tumewafundisha matumizi ya mfumo wa usajili wa maduka ya bidhaa za chakula na vipodozi unaojulikana kama ‘Online Application System’ (OAS). Mfumo huu utawasaidia kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi, tuna matumaini kwamba baada ya mafunzo haya, Jiji la Dodoma litaendelea kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya ushirikiano kati ya TBS na Mamlaka za Serikali za Mitaa (LGA), na kuwa mfano wa kuigwa kitaifa, sambamba na kaulimbiu yao ya kwamba 'Dodoma Inapaa',” alisema Lutahala.

Alisema kuwa mbali na kuwajengea uwezo, mafunzo hayo yamekusudia kuwasaidia wahusika hao kupiga hatua katika utekelezaji wa majukumu yao kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa.







 

Comments

Popular Posts

Barabara za Mtaa wa Mbwanga yafunguliwa, Diwani Kerenge aitaja kuwa chachu ya maendeleo

Dodoma Jiji yajiandaa Ngoma na Kwaya SHIMISEMITA, 2026

Kanda Namba Tatu yaimarisha ushirikiano na wamiliki wa vituo vya malezi ya watoto Dodoma