Wazazi wahimizwa kufuatilia elimu na tabia za watoto nyumbani
Na. Mwandishi wetu, DODOMA
Wazazi
wamehimizwa kuwa na ushirikiano wa karibu na walimu katika kufuatilia maendeleo
ya watoto wao wanapokuwa nyumbani, ili kusaidia kukuza uwezo wao kitaaluma na
kujenga msingi bora wa elimu, badala ya kutegemea walimu pekee katika jukumu
hilo.
Wito huo ulitolewa
na Mwalimu Mkuu wa Shule ya Shekinah Pre & Primary School, Obadia Mwambapa
wakati wa siku maalumu ya kufunga shule, ambapo alisema kuwa ushirikiano kati
ya wazazi na walimu ni muhimu katika kuhakikisha watoto wanapata malezi na
elimu bora.
Alisema kuwa wazazi
wanapaswa kutenga muda wa kufuatilia masomo ya watoto wao, kujua changamoto
wanazokutana nazo na kushirikiana na walimu katika kutafuta suluhisho.
Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Shule hiyo,
Juliana Sabrere alisema kuwa ulinzi na usalama wa watoto ni jukumu la pamoja
kati ya walimu na wazazi, akisisitiza umuhimu wa kushirikiana katika kulinda
maadili mema ya watoto na kuhakikisha wanakua katika mazingira salama na yenye
malezi yanayozingatia misingi ya heshima, uwajibikaji na nidhamu.
Alisema kuwa malezi bora ya watoto yanahitaji ushiriki wa pande zote mbili, kwa kuwa mtoto anahitaji uangalizi na mwongozo akiwa shuleni na nyumbani.
Aidha, aliwataka wazazi na walimu kuwa karibu na watoto, kuwasikiliza na
kuwasaidia kutambua mambo mema na mabaya ili kujenga kizazi bora cha sasa na
cha baadaye.
Comments
Post a Comment