Serikali yafikisha Umeme katika maeneo 582 ya wachimbaji wadogo, kilimo na viwanda Tanzania bara

Na. Mwandishi wetu, DODOMA

 

Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba, amesema Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imetekeleza Mradi wa Usambazaji Umeme katika maeneo 582 ya wachimbaji wadogo, kilimo na viwanda Tanzania Bara, kwa gharama ya shilingi bilioni 115.

 


Makamba aliyasema hayo bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mwanahamisi Athumani, Mbunge wa Viti Maalumu, aliyetaka kujua ni lini serikali itatekeleza Mpango Mkakati Maalumu wa kuhakikisha maeneo ya wachimbaji wadogo yanafikishiwa umeme wa kutosha kwa lengo la kupunguza gharama za uzalishaji.

 

Akijibu swali hilo, Makamba alisema kuwa mradi huo ulianza kutekelezwa Aprili, 2023 na kwa sasa umefikia hatua za mwisho za utekelezaji.

Aidha, alisema kuwa Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na Wizara ya Madini inaendelea kuainisha maeneo ya kipaumbele yatakayofikishiwa huduma ya umeme katika hatua zinazofuata, kwa kuzingatia upatikanaji wa fedha.

 

Sambamba na hilo, alisema kuwa serikali kupitia TANESCO, kwa kutumia fedha za ndani, inaendelea kutekeleza miradi ya kuimarisha miundombinu ya usafirishaji na usambazaji wa umeme pamoja na ujenzi na uboreshaji wa vituo vya kupoza umeme katika mikoa mbalimbali nchini, hususan maeneo yenye changamoto ya low voltage.

 

Alisema kuwa hatua hizo ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha maeneo yote ya uzalishaji yanafikiwa na huduma ya umeme ya kutosha na ya uhakika.

 

Makamba alisisitza kuwa lengo la serikali ni kuhakikisha wachimbaji wadogo, wakulima, viwanda na maeneo mengine ya uzalishaji yanapata umeme wa kutosha na wa uhakika wakati wote, ili kupunguza gharama za uzalishaji, kuongeza tija na kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi nchini.

 

 

Comments

Popular Posts

Wafanyabiashara Soko la Miembeni Waazimia Kulinda Usafi

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lapitisha taarifa ya ufungaji hesabu 2025/2026

Wilaya ya Dodoma kuchanja watoto zaidi ya laki 2 chanjo ya Polio