NW. Salome: Wizara ya Nishati ina wajibu wa kuhakikisha wananchi wanapata Umeme wa uhakika

Na. Mwandishi wetu, DODOMA

Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba amesema jukumu kuu la Wizara ya Nishati ni kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika na wanapatiwa taarifa kwa wakati pindi changamoto zinapojitokeza.



Makamba aliyasema hayo wakati akijibu swali la Exaud Kigahe, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kaskazini aliyetaka kufahamu lini serikali itabadilisha mkataba wa usambazaji wa umeme kwa wananchi kutoka Mwenga Power kwenda TANESCO, ili Mwenga Power ibaki kuwa mzalishaji wa umeme.

Akijibu swali hilo, Makamba alisema kuwa utoaji na usimamizi wa leseni za uzalishaji na usambazaji wa umeme nchini ni jukumu la kisheria la Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA), kwa mujibu wa Sheria ya Umeme ya mwaka 2008 na taratibu za utoaji wa leseni hizo.

“Jukumu namba moja la Wizara ya Nishati ni kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika na wanapata taarifa kwa wakati kunapotokea changamoto,” alisema Makamba.

Alieleza kuwa uamuzi wowote wa kubadili muundo wa leseni ya usambazaji umeme katika eneo hilo unapaswa kuzingatia matakwa ya sheria na taratibu zilizowekwa.

Hata hivyo, Makamba alisema kuwa serikali, kwa kutambua kuwa kumekuwa na malalamiko kuhusu ubora wa huduma inayotolewa na Mwenga Power, tayari taasisi zake za EWURA, TANESCO na REA zimeanza kufanya tathmini ya kina ili kubaini uwezekano wa kufanya mabadiliko hayo bila kuathiri uwekezaji uliopo.

Alisema kuwa tathmini hiyo itafanyika kwa haraka ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme yenye uhakika na inayokidhi mahitaji yao.

Alisema yupo tayari, pindi vikao vya Bunge vitakapokamilika, kuongozana na Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kaskazini, kwenda kusikiliza na kufahamu kwa kina changamoto zinazowakabili wananchi katika eneo hilo.

 

Comments

Popular Posts

Baraza la Madiwani Jiji la Dodoma lapitisha taarifa ya ufungaji hesabu 2025/2026

Wilaya ya Dodoma kuchanja watoto zaidi ya laki 2 chanjo ya Polio