Prof. Nagu awataka wananchi kuzingatia Lishe bora kukuza Uchumi
Na. Mwandishi wetu, DODOMA
WANANCHI wametakiwa kuzingatia ulaji bora wa chakula
kwa ajili ya kuboresha na kulinda afya kwa kutumia mazao yanayozalishwa katika Halmashauri
ya Jiji la Dodoma ili wawe na lishe bora itakayowasaidia kutekeleza majukumu ya
kujenga taifa.
Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anayeshughulikia masuala ya Afya, Prof. Tumaini Nagu alipotembelea banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika maonesho ya Nanenane yanayoendelea jijini Dodoma.
Prof. Nagu aliwasisitiza wananchi kuzingatia ulaji wa
chakula bora kwa ajili ya afya bora, akisema kuwa mazao yanayozalishwa katika
Jiji la Dodoma ni bora na yanamchango mkubwa katika kuboresha lishe. “Niwapongeze
Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kazi nzuri mnayoifanya. Pia niwasisitize wananchi
hasa vijana kula chakula bora kama tulivyojionea hapa. Mazao yanayozalishwa ni
mazao bora kabisa kwa afya. Hivyo, vijana kama kizazi cha baadae wajitahidi
kula chakula bora kwa kuzingatia lishe, jambo litakalowasaidia kutekeleza wajibu
wao katika kujenga taifa imara” alisema Prof. Nagu.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu OWM-TAMISEMI,
Sospeter Mtwale aliipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kazi nzuri
inayofanya katika kuendeleza kilimo na kubuni fursa mbalimbali za maendeleo.
Awali akitoa maelezo kwa viongozi hao walipotembelea banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma Afisa Kilimo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Clementina Kabaka aliwaelezea juu ya kilimo cha mazao mbalimbali yanayozalishwa jijini hapo, namna ya kuongeza thamani ya mazao pamoja na kuonesha mazao yanayolimwa yakiwepo mazao yanayostawi katika maeneo yenye hali ya hewa ya baridi.
Vilevile, alieleza miradi mbalimbali inayotekelezwa na
Halmashauri ya Jiji la Dodoma na kuelezea fursa za uwekezaji zilizopo, hususan
katika sekta ya kilimo na uzalishaji wa mazao yenye tija kwa wananchi.
Comments
Post a Comment