Dodoma Jiji FC yajiwinda dhidi ya Namungo dimba la Jamhuri

Na. Amoni Sambulila, DODOMA

Timu ya Dodoma Jiji FC imeendelea na maandalizi kuelekea mchezo wa raundi ya sita wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara dhidi ya Timu ya Namungo FC, utakaochezwa leo Ijumaa majira ya saa moja usiku katika Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma.



Akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari kuelekea mchezo huo, Kocha Mkuu wa Timu ya Dodoma Jiji FC, Vicent Mashami alisema kuwa timu yake ipo katika hali nzuri baada ya kupata ushindi katika michezo miwili iliyopita, huku akisisitiza umuhimu wa kuendeleza mwenendo huo wa ushindi.

“Timu ipo vizuri, ambapo mechi mbili zilizopita tulipata ushindi na hivyo tunahitaji kuwa na mwendelezo wa ushindi. Pia Namungo ni timu yenye ubora na ushindani, licha ya kupoteza mechi tatu zilizopita, hivyo tunatambua mchezo huu hautakuwa rahisi,” alisema Mashami.

Kwa upande wake, mchezaji Mwanakibuta David, alisema kuwa wachezaji wako tayari kupambana katika mchezo huo na kuhakikisha wanaendelea kupata matokeo mazuri.

“Tunajua mchezo dhidi ya Timu ya Namungo utakuwa na ushindani, lakini sisi tumejiandaa vizuri na tunahitaji kuendelea na mwenendo mzuri tuliouanza katika michezo miwili iliyopita,” alisema Mwanakibuta.

Dodoma Jiji FC inaingia katika mchezo huo ikiwa na dhamira ya kuendeleza matokeo mazuri baada ya kupata ushindi katika michezo miwili iliyopita, huku Namungo FC ikitafuta kurejea kwenye matokeo mazuri baada ya kupoteza michezo yake mitatu iliyopita.

Comments

Popular Posts

Wafanyabiashara Soko la Miembeni Waazimia Kulinda Usafi

Kata ya Miyuji Yaongeza Kasi ya Usimamizi Wa Usafi wa Mazingira

Vijana Dodoma na Iringa Kukutana Kupaza Sauti Dhidi ya Rushwa