TARURA Dodoma yatakiwa kukamilisha miradi kwa wakati
Na. Coletha Charles, NZUGUNI
Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA)
wametakiwa kukamilisha kwa wakati, miradi ya uboreshaji wa barabara yenye urefu
wa kilomita 3.8 kwa kuzingatia ubora na thamani ya fedha ili iweze kuleta
manufaa yaliyokusudiwa kwa wananchi wa Jiji la Dodoma.
Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj
Jabir Shekimweri, wakati wa ziara ya kutembelea na kukagua maendeleo ya mradi huo,
ikiwa ni sehemu ya hatua za kukabiliana na athari za mvua za El Nino.
Alisema kuwa utekelezaji wa mradi huyo unapaswa kwenda
sambamba na usimamizi madhubuti wa muda, ubora wa kazi na matumizi sahihi ya
fedha, ili wananchi wa Jiji la Dodoma wanufaike na miundombinu hiyo kwa muda
uliokusudiwa.
“Ninawasihi TARURA kuhakikisha mradi huu unakamilishwa
kwa wakati na kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa, ili wananchi waweze kupata
manufaa yaliyokusudiwa. Muhimu ni kuhakikisha fedha zinazotumika katika mradi
huu zinatoa thamani halisi kwa wananchi,” alisema Alhaj Shekimweri.
Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Meneja wa
TARURA Wilaya ya Dodoma, Mha. Emmanuel Mfinanga alisema kuwa mradi huo inahusisha
Barabara ya Nzuguni kwa Masista yenye urefu wa kilomita 0.5 kwa kiwango cha
lami, pamoja na Nzuguni Makaburini yenye urefu wa kilomita 1.5 kwa kiwango cha
changarawe yenye gharama ya shilingi 694,144,950, huku chanzo cha fedha kikiwa
ni Road Fund Development.
Alisema kuwa TARURA inatekeleza mradi wa Barabara ya
Mwangaza yenye urefu wa kilomita 1.1 kwa kiwango cha lami, wenye thamani ya shilingi
1,630,184,137.91, pamoja na Barabara ya Mwangaza Mwambosa yenye urefu wa
kilomita 0.7 kwa kiwango cha lami, wenye thamani ya shilingi 880,120,820.12
bila VAT.
“Mradi wa Barabara ya Mwangaza umefikia asilimia 55 ya
utekelezaji dhidi ya asilimia 30 ya muda uliotumika, huku Mwangaza Mwambosa ukiwa
imefikia asilimia 70 ya utekelezaji dhidi ya asilimia 52.70 ya muda
uliotumika,” alisema Mha. Mfinanga.
Kwa ujumla, utekelezaji wa miradi hiyo unatarajiwa
kuongeza ubora wa miundombinu ya barabara katika Jiji la Dodoma, kurahisisha
usafiri na usafirishaji wa bidhaa, pamoja na kupunguza changamoto
zinazowakabili wananchi wakati wa mvua.
MWISHO
Comments
Post a Comment