DC Shekimweri aagiza kampeni maalum ya usafi kukabiliana na El Nino
Na. Coletha Charles, NZUGUNI
TANROADS, TARURA, DUWASA na Serikali za Mitaa katika
Halmashauri ya Jiji la Dodoma zimetakiwa kuendesha kampeni maalum ya usafi wa
mitaro, makalavati na madaraja katika kipindi cha Mwezi Agosti, Septemba na
Oktoba, 2026 ili kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na mvua kubwa za El
Nino.
Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma,
Alhaj Jabir Shekimweri katika viwanja vya Dkt. John Malecela Kata ya Nzuguni,
wakati wa utekelezaji wa maelekezo ya serikali ya kuchukua hatua za mapema
kukabiliana na athari zinazoweza kusababishwa na mvua zitakazonyesha kwa
kiwango cha juu ya wastani.
Alhaj Shekimweri alisema kuwa mvua nyingi huleta
athari katika makazi ya watu kutokana na kuzibwa kwa mitaro, makalavati na
madaraja, hususan kwa taka na michanga.
“TANROADS na TARURA, mnatakiwa kutangulia mkafanye
ukaguzi wa hiyo miundombinu ya barabara. Na mimi nitapenda kupewa taarifa ya
ukaguzi wenu umebainisha wapi na wapi na kama kuna changamoto kubwa hatua za
haraka zichukuliwe. Pengine na sisi tukaongeza nguvu. Ni muhimu sana
kushirikiana na serikali za mitaa kwenye jambo hili. Itakapobidi kutumia
rasilimali, zitumike kwa uangalifu,” alisema Alhaj Shekimweri.
Aidha, alieleza kuwa DUWASA inapaswa kushirikishwa
katika maeneo yenye changamoto ya maji na majitaka, akitolea mfano eneo la Kitelela,
Nzuguni ambako kumekuwa na changamoto ya mwingiliano wa majitaka na maji safi.
Pia, vijana wanaweza kushirikishwa katika kufanya usafi huo, lakini wanapaswa
kupewa vifaa vya kazi na vya usalama kulingana na mazingira watakayofanyia
kazi.
Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Matengenezo
TANROADS Mkoa wa Dodoma, Mha. Filbert Biseko alisema kuwa wakala huo umejipanga
kukabiliana na El Nino kwa kusafisha mitaro, kutengeneza barabara na kuandaa
mkandarasi wa dharura.
“Kwa sehemu kubwa ya mjini hapa, tayari tumeshafanya ‘procurement’
kwa ajili ya kuwapata wakandarasi ambao wataanza kufanya kazi za kusafisha
mitaro. Lakini pia, kuna zile barabara ambazo zina changamoto, tayari tumeshapata
wakandarasi,” alisema Mha. Biseko.
Nae, Meneja wa TARURA Wilaya ya Dodoma, Mha. Emmanuel
Mfinanga, alisema kuwa TARURA iko katika hatua za mwisho za kumpata mkandarasi
wa kujenga daraja katika eneo la Kitelela, Nzuguni, ambako watoto wamekuwa
wakipata changamoto kuvuka wakati wa mvua.
“Nakumbuka mwaka jana tulitembelea barabara ya
Kitelela, kule Nzuguni. Kuna eneo ambalo watoto walikuwa wanavuka kwa shida,
bahati nzuri tuliweka kwenye bajeti na tayari tuko hatua za mwisho kumpata
mkandarasi ili akajenge ile daraja na kutengeneza ile barabara,” alisema Mha. Mfinanga.
Hata hivyo, Diwani wa Kata ya Nzuguni, Leonard Ndama
alisema kuwa hatua hizo za serikali ni muhimu katika kujiandaa na msimu wa mvua
na kuwalinda wananchi dhidi ya madhara yanayoweza kujitokeza.
“Nimefarijika kuona serikali ikichukua hatua mapema.
Hii inaonesha kwamba serikali inafanya kazi na inajali usalama wa wananchi,
hasa katika kukabiliana na changamoto zinazoweza kusababishwa na mvua,” alisema
Ndama.
Utekelezaji wa ukaguzi na usafi wa mitaro, makalavati na
madaraja kabla ya msimu wa mvua unatarajiwa kupunguza hatari ya mafuriko na
kulinda maisha pamoja na mali za wananchi. Ushirikiano kati ya TANROADS,
TARURA, Serikali za Mitaa, DUWASA na wananchi utakuwa muhimu katika kuhakikisha
maandalizi hayo yanafanikiwa.
MWISHO
Comments
Post a Comment