DC Shekimweri aagiza kuzingatia usalama maeneo ya uchimbaji madini ujenzi

Na. Coletha Charles, NZUGUNI

Ofisi ya Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma imetakiwa kuandaa orodha ya maeneo yote yaliyotolewa vibali vya uchimbaji wa madini ya ujenzi, kubaini yaliyo katika matumizi, yaliyokamilisha shughuli za uchimbaji na yale ambayo hayajarejeshwa katika hali salama.



 

Agizo hilo limetolewa katika Ofisi ya Utawala viwanja vya Dkt. John Malecela, Nzuguni na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri katika kikao cha maandalizi ya kukabiliana na athari za mvua za El Nino.

 

Alhaj Shekimweri alisema kuwa waendeshaji wa maeneo hayo wanapaswa kutekeleza mpango wa ‘Environmental Management Plan’ (EMP) iliyowekwa wakati wa utoaji wa vibali, ikiwemo kusawazisha na kurejesha maeneo hayo katika hali salama baada ya kumaliza uchimbaji.

 

“Tupate taarifa wangapi wamezingatia ile EMP na kuweka maeneo hayo kama inavyotakiwa kwenye EMP na wangapi hawajafanya. Wale ambao hawajafanya, mnipe orodha lakini muwe tayari mmesha waandikia barua. Nataka tarehe moja mwezi wa Oktoba, 2026 tupite na Kamati ya Maafa tukakague hayo maeneo,” alisema Alhaj Shekimweri.

 

Alisema kuwa waendeshaji ambao watabainika kutotekeleza masharti ya EMP watachukuliwa hatua za kisheria. Pia, aliwataka maafisa watendaji wa kata na mitaa kushirikiana na serikali katika kubaini maeneo yaliyotelekezwa na kutoa taarifa ili hatua zichukuliwe mapema.

 

“Nikikuta kuna eneo ambalo halijafanyiwa kazi kwa mujibu wa EMP, huyo aliyepewa leseni tutamshitaki. Lakini kwa yale maeneo makubwa ambayo ‘restoration’ yake itachukua muda, yawekwe uzio, milango au alama za tahadhari ili kuzuia watu kuingia, huku yale madogo yakirejeshwa katika hali salama kwa haraka,” alisema.

 

Kwa upande wake, Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Wilaya ya Dodoma, Insp. Deogratus Peter, alisema kuwa wazazi na walezi wanapaswa kuwaelimisha watoto kuepuka maeneo hayo kutokana na hatari iliyopo, huku watendaji wa kata na mitaa wakitakiwa kuweka alama za tahadhari na kuendelea kutoa elimu kwa wananchi.

 

“Ningeomba sana yale maeneo yote kwanza tuweze kuyatambua. Yale maeneo ambayo wakandarasi wetu tuliwapa zile kandarasi kwa ajili ya kwenda kuchukua madini ya ujenzi, tujue tunazifanyaje ‘restoration’. Kama tutashindwa labda kutokana na ‘issues’ za bajeti, basi tuangalie namna ya kuweza ‘kuzisecure’, kuziwekea ‘cordon tape’,” alisema Insp. Peter.

 

Kwa hatua hizo, serikali inalenga kuzuia ajali na vifo vinavyoweza kusababishwa na mashimo ya uchimbaji kujaa maji wakati wa mvua, huku wamiliki wa maeneo hayo wakitakiwa kutekeleza masharti ya mazingira na kurejesha maeneo katika hali salama.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Vijana watakiwa kujiendeleza nje ya mfumo rasmi

NGOs zatakiwa kuzingatia uwazi na uwajibikaji Dodoma