Dodoma CC Yatwaa Ubingwa wa Mpira wa Mikono SHIMISEMITA, 2026

Na. Leah Mabalwe, MBEYA

 

Timu ya Mpira wa Mikono ya Wanaume kutoka Halmashauri ya Jiji la Dodoma imetwaa ubingwa wa mashindano ya SHIMISEMITA yanayofanyika jijini Mbeya, baada ya kuicharaza Halmashauri ya Wilaya ya Geita magoli 9-6 katika mchezo wa fainali.


 

Mchezo huo wa kusisimua ulifanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari Samora, ambapo timu zote mbili zilionesha ushindani mkubwa katika kuwania taji hilo.

 

Akizungumza mara baada ya mchezo huo, Kocha wa Timu ya Mpira wa Mikono ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Baraka Muhamed alisema kuwa mchezo huo ulikuwa mgumu kutokana na timu zote mbili kuwa zilijiandaa vizuri kwa ajili ya kuwania ubingwa. “Mchezo ulikuwa mgumu kwa sababu pande zote mbili zilikuwa zimejipanga vizuri kwa ajili ya kuwania ubingwa huu. Tumejituma sana hadi kufikia hatua hii. Nawashukuru sana wachezaji wote kwa kujituma na kutupa ushindi huu” alisema Muhamed.

 

Kwa upande wake, Nahodha wa Timu hiyo, Charles Malima alisema kuwa wamepata furaha kubwa baada ya kutimiza ahadi waliyompa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

“Tuna furaha kubwa sana kwa sababu kile tulichomuahidi mkurugenzi wetu sasa kimetimia. Pia tunafuraha sana kufika hatua hii, kwa sababu mwaka jana tulikuwa washindi wa pili, lakini mwaka huu tumetimiza lengo letu la kuwa mabingwa” alisema Malima.

 

Nae shabiki wa michezo kutoka jijini Mbeya, Ibrahim Masauti aliipongeza timu ya Mpira wa Mikono ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kiwango ilichoonesha katika mashindano hayo, akisema kuwa ushindi wa magoli 9-6 katika mchezo wa fainali si jambo dogo. “Halmashauri ya Jiji la Dodoma wapo vizuri. Kushinda magoli 9-6 katika mchezo wa fainali si mchezo. Dodoma Jiji ipo vizuri. Hivyo, nawashauri halmashauri nyingine zijifunze na kuwekeza zaidi katika michezo kupitia mfano wa Dodoma Jiji” alisema Masauti.

Ushindi huo unaifanya Halmashauri ya Jiji la Dodoma kuandika historia mpya katika mashindano hayo, baada ya kushindwa kutwaa ubingwa huo mwaka jana na kumaliza katika nafasi ya pili. Mwaka huu, timu hiyo imefanikiwa kupanda hatua moja zaidi na kuondoka na taji la ubingwa.

Comments

Popular Posts

Vijana watakiwa kujiendeleza nje ya mfumo rasmi

NGOs zatakiwa kuzingatia uwazi na uwajibikaji Dodoma