NGO’s Wilaya ya Dodoma wahimizwa ushirikiano

Na. Rahma Magona, DODOMA

Mashirika yasiyo ya kiserikali wilayani Dodoma yameaswa kuimarisha ubia, ubunifu na matumizi ya vyanzo vya ndani vya rasilimali fedha ili kuongeza uendelevu wa shughuli zao na kutoa mchango zaidi katika maendeleo ya jamii.


Rai hiyo ilitolewa katika mkutano wa Jukwaa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali wilayani Dodoma uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, ambapo mgeni rasmi alikuwa mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Joan Mazanda ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Uchumi, Elimu na Afya Halmashauri ya Jiji Dodoma.

Akizungumza katika mkutano huo, alisema kuwa mashirika yasiyo ya kiserikali yanachangia katika kujenga ushirikiano na kuibua fikra endelevu zinazolenga kuimarisha maendeleo ya wananchi. Vilevile, aliongeza kuwa mashirika hayo yamekuwa yakitekeleza shughuli mbalimbali katika jamii, zikiwemo afua za afya na mazingira, pamoja na kutoa misaada kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu.

Kwa upande wake mmoja wa mshiriki kutoka Taasisi ya Binti Salama, Faith William alisema kuwa mkutano huo umesaidia katika kukutanisha wadau, kufahamiana, kupata elimu na kufahamu fursa zilizopo.

Mkutano huo umejadili masuala mbalimbali yanayohusu uendelevu wa mashirika yasiyo ya kiserikali, ubunifu, ujenzi wa ubia pamoja na upatikanaji wa rasilimali fedha kupitia vyanzo vya ndani, kwa lengo la kuimarisha mchango wa mashirika hayo katika maendeleo ya jamii.

 

Comments

Popular Posts

Vijana watakiwa kujiendeleza nje ya mfumo rasmi

NGOs zatakiwa kuzingatia uwazi na uwajibikaji Dodoma

Ziara ya DC kukagua ujenzi wa Barabara Dodoma