Dodoma yasisitiza Elimu nje ya mfumo rasmi

Na. Rahma Magona, DODOMA

Juma la Elimu ya Watu Wazima na Elimu Nje ya Mfumo Rasmi limefikia kilele leo katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma, huku serikali ikisisitiza umuhimu wa kuimarisha fursa za elimu kwa wananchi ambao hawakupata nafasi ya kusoma katika mfumo rasmi.



Akizungumza katika maadhimisho hayo, mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma ambae ni Katibu Tawala Msaidizi anayeshughulikia elimu, Kiduma Mageni alisema kuwa serikali imeendelea kuwekeza katika uimarishaji wa miundombinu ya elimu ili kuhakikisha wananchi wanapata fursa ya kujifunza.

 

Alisema kuwa Mkoa wa Dodoma ulipokea zaidi ya shilingi bilioni 22 kwa ajili ya uimarishaji wa miundombinu ya elimu, hatua inayolenga kuhakikisha kila mwanafunzi anapata fursa ya kupata elimu katika mfumo rasmi.

 

Vilevile, wananchi ambao walishindwa kupata elimu katika mfumo rasmi bado wana nafasi ya kuendelea na masomo kupitia elimu nje ya mfumo rasmi kwa kutumia miundombinu iliyopo, aliongeza.

 


Kwa upande wake Witness Isaya alisema kuwa elimu nje ya mfumo rasmi ni muhimu kwa kuwa inatoa nafasi kwa wananchi ambao hawakupata elimu katika mfumo rasmi kuendelea kujifunza na kupata ujuzi unaoweza kuwasaidia katika shughuli zao za kila siku.

 

Maadhimisho hayo yameendelea kusisitiza umuhimu wa elimu kwa kila mwananchi bila kujali umri au mazingira yake, huku jamii ikihimizwa kutumia fursa za elimu zinazopatikana ili kuongeza maarifa, ujuzi na kuchangia maendeleo ya mtu binafsi pamoja na jamii kwa ujumla.

Comments

Popular Posts

Vijana watakiwa kujiendeleza nje ya mfumo rasmi

NGOs zatakiwa kuzingatia uwazi na uwajibikaji Dodoma