Uendelevu wa NGOs wapatiwa msukumo wilayani Dodoma

Na. Amoni Sambulila, DODOMA

 

Halmashauri ya Jiji la Dodoma kupitia Jukwaa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali imeendelea kutoa msukumo kwa mashirika hayo kuimarisha uendelevu wa shughuli na miradi wanayoitekeleza, ili kuhakikisha huduma zinazotolewa zinaendelea kuwa na manufaa kwa jamii kwa muda mrefu.

 


Akizungumza katika mkutano wa Jukwaa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali uliofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Afisa Maendeleo ya Jamii katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Ester Erick alisema kuwa uendelevu wa mashirika hayo ni muhimu katika kuhakikisha miradi na huduma zinazotekelezwa kwa ajili ya wananchi zinaendelea kutoa matokeo chanya.

 

Alisema kuwa katika kipindi cha utekelezaji, jumla ya miradi 30 ilitekelezwa katika maeneo mbalimbali, ikiwemo afya, elimu, utunzaji wa mazingira, msaada wa kisheria pamoja na shughuli zinazohusisha Dawati la Jinsia.

 

“Jumla ya miradi 30 imetekelezwa katika maeneo ya afya, elimu, utunzaji wa mazingira, msaada wa sheria na Dawati la Jinsia, kwa gharama ya shilingi milioni 180.87 na kuwafikia wanufaika 23,632, kati yao wanaume ni 6,001, wanawake ni 7,419 na watoto 10,212” alisema Erick.

 

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Rise up Integrity for Human Support (RIHS), John Malale alisema kuwa ushirikiano kati ya serikali, mashirika yasiyo ya kiserikali na wadau wengine ni muhimu katika kuhakikisha miradi inayotekelezwa inaleta matokeo yenye tija na endelevu kwa jamii.

 


Nae Mkurugenzi Mkuu wa God Bless Network Foundation, Julius Kilabuka alisema kuwa mashirika yasiyo ya kiserikali yanapaswa kuendelea kuimarisha uwezo wao wa kiutendaji pamoja na kujenga ushirikiano madhubuti na wadau mbalimbali ili kuhakikisha huduma zinazotolewa kwa wananchi zinaendelea kwa ufanisi.

 


Mkutano huo ulilenga kujadili utekelezaji wa shughuli za mashirika yasiyo ya kiserikali, ufuatiliaji wa miradi inayotekelezwa pamoja na kuweka mikakati ya kuimarisha uendelevu wa huduma zinazotolewa kwa jamii.

Comments

Popular Posts

Vijana watakiwa kujiendeleza nje ya mfumo rasmi

NGOs zatakiwa kuzingatia uwazi na uwajibikaji Dodoma