Timu ya Jiji la Dodoma yajinoa kuelekea SHIMISEMITA Mbeya, 2026
Na. Mwandishi Wetu, Dodoma
MSAKO
wa kutetea ubingwa wa mashindano ya Shirikisho la Michezo la Serikali za Mitaa
Tanzania (SHIMISEMITA) umeanza rasmi kwa Halmashauri ya Jiji la Dodoma baada ya
watumishi wake kushiriki bonanza la michezo lililozikutanisha Halmashauri ya
Jiji la Dodoma, Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino na Halmashauri ya Wilaya ya Gairo
katika Uwanja wa Shule ya Sekondari Dodoma.
Bonanza hilo limekuwa sehemu ya maandalizi ya kuelekea mashindano ya SHIMISEMITA yanayotarajiwa kufanyika mwezi Agosti mwaka huu jijini Mbeya, ambapo halmashauri mbalimbali nchini zitachuana kuwania ubingwa katika michezo tofauti.
Akizungumza
baada ya bonanza hilo, Afisa Michezo wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Neema
Kilongola alisema kuwa maandalizi yanaendelea vizuri na mechi hizo zimewapa
nafasi ya kupima uwezo wa kikosi kabla ya kuelekea Mbeya. “Bonanza hili
limetupa nafasi ya kujipima, kurekebisha mapungufu na kuongeza ushindani ndani
ya timu. Mwaka jana tulikuwa mabingwa, hivyo mwaka huu tunakwenda Mbeya kutetea
ubingwa wetu kwa nguvu zote,” alisema Kilongola.
Kwa
upande wake, Mchezaji wa Mpira wa Mkono, Mwidini Mwenda, alisema kuwa morali ya
wachezaji iko juu na kila mmoja amedhamiria kupambana ili kuendelea kuipeperusha
vema bendera ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma. “Maandalizi yanaendelea vizuri
na kila mchezaji anajituma kuhakikisha timu inakuwa katika kiwango bora.
Tunafahamu ushindani utakuwa mkubwa, lakini tumejipanga kurudi Dodoma na
ushindi kama ilivyokuwa mwaka uliopita,” alisema Mwenda.
Mashindano
ya SHIMISEMITA 2026 yanatarajiwa kuzikutanisha halmashauri kutoka maeneo
mbalimbali nchini, huku Halmashauri ya Jiji la Dodoma ikiingia katika
mashindano hayo ikiwa na dhamira ya kutetea ubingwa wake.
Comments
Post a Comment