Wilaya ya Dodoma kutumia vyombo vya habari katika kampeni ya dhidi ya chanjo ya Polio

Na. Coletha Charles, NKUHUNGU

Wilaya ya Dodoma imeweka mkakati wa kutumia vyombo vya habari, viongozi wa dini, shule na kampuni za simu ili kuwahamasisha wazazi kuwapeleka watoto kupata chanjo salama dhidi ya ugonjwa wa Polio, lengo likiwa ni kutokomeza kabisa hatari ya maambukizi ya ugonjwa huo.



Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa zoezi hilo katika Shule ya Msingi Nkuhungu, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri, alisema kuwa vipindi vya redio na televisheni, hususani vipindi vya asubuhi, vitatumika kutoa elimu kwa wananchi na kujibu maswali kuhusu umuhimu na usalama wa chanjo hiyo.

Alisema kuwa viongozi wa dini nao wamepewa nafasi muhimu katika uhamasishaji huo, kutokana na ushawishi wao katika jamii na uwepo wa watoto katika maeneo ya ibada, ikiwemo ‘Sunday Schools’, madrasa na jumuiya mbalimbali za kidini.

“Tumeona pia kupitia eneo hilo kila mtoto wa Tanzania apate nafasi ya kupata chanjo hiyo. Tumewahamasisha shule zote, kamati na bodi za shule kufikisha ujumbe kwa wazazi. Pia tumeandaa ujumbe mfupi kwa kushirikiana na Vodacom, Tigo na Airtel ili kuwafikishia wananchi taarifa kuhusu zoezi hili kupitia simu zao,” alisema Alhaj Shekimweri.



Aidha, shule zimeingizwa katika mpango huo wa uhamasishaji, ambapo alisema wasimamizi wapatao 911 walioshiriki katika semina ya mitihani wamepewa maelekezo ya kuhakikisha kamati na bodi za shule zinawafikishia wazazi taarifa kuhusu zoezi hilo.

Kwa upande wake, Afisa kutoka Wizara ya Afya, Idara ya Kinga sehemu ya Elimu ya Afya, Magdalena Dinawi, alisema kuwa lengo la kampeni hiyo ni kuongeza na kuimarisha kinga ya watoto dhidi ya virusi vya Polio aina ya pili, kuzuia maambukizi kwa binadamu kupitia mazingira na kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa nchi isiyo na maambukizi ya Polio.

“Natoa wito kwa wazazi na walezi kuhakikisha mtoto anapata chanjo hata kama tayari ameshapata chanjo ya Polio kliniki au katika kampeni zilizopita. Chanjo ni kinga, mpe chanjo, mlinde mtoto. Pia chanjo hii inatolewa bila malipo katika vituo vya kutolea huduma za afya, nyumba kwa nyumba, tutatoa pia katika nyumba zetu za ibada, vituo vya mabasi, sokoni na maeneo yote ya mikusanyiko ambapo anapatikana mtoto chini ya miaka 10,” alisema Dinawi.



Nae, Mkazi wa Kata ya Nkuhungu, Mtaa wa Itega, Ally Hassan aliwasihi wazazi wenzake kutopuuza huduma hiyo inayotolewa bure na badala yake wawapeleke watoto wao ili kulinda afya na maisha yao ya baadaye.

 

“Natoa wito kwa wazazi na walezi wahakikishe mtoto anapata chanjo hata kama tayari alishapata chanjo ya Polio kliniki au katika kampeni zilizopita. Kupata chanjo katika kampeni hii kunaongeza na kuimarisha kinga ya mwili na hivyo kumpa mtoto ulinzi dhidi ya virusi vya polio vinavyoweza kuwepo kwenye mazingira” alisema.

Mkakati huo umetajwa kuwa muhimu katika kuhakikisha ujumbe wa chanjo kulingana na Kaulimbiu ‘Mpe chanjo mtoto wako, linda tabasamu la mtoto, zuia Polio’ unawafikia wananchi kwa wakati, ikizingatiwa kuwa sehemu kubwa ya wakazi wa mijini hutumia usafiri wa umma kwenda kazini na hivyo kupata fursa ya kusikiliza redio wakiwa safarini

Comments

Popular Posts

Vijana watakiwa kujiendeleza nje ya mfumo rasmi

NGOs zatakiwa kuzingatia uwazi na uwajibikaji Dodoma

Ziara ya DC kukagua ujenzi wa Barabara Dodoma