Wananchi washauriwa kushirikiana na wataalam wa Afya kufanikisha Kampeni ya Chanjo ya Polio
Na. Mwandishi wetu, DODOMA
Wananchi wametakiwa kushirikiana na
wataalamu wa afya katika utekelezaji wa kampeni ya chanjo ya Polio itakayoanza tarehe
27-30 Agosti, 2026, zoezi hilo litafanyika nyumba kwa nyumba pamoja na katika
maeneo yenye mikusanyiko ya watoto na katika vituo vya kutolea huduma za afya.
Akizungumza katika kipindi cha Password ya leo kupitia Manyunyu TV, Mganga Mkuu wa Jiji la Dodoma, Dkt. Pima Sebastian alisema kuwa kampeni hiyo inalenga kuhakikisha hakuna mtoto anayekosa fursa ya kupata chanjo ya Polio. Aliongeza kuwa timu za afya zitawafikia watoto nyumbani. Maeneo mengine aliyoyataja kuwa yatafikiwa ni katika masoko, shule za msingi, vituo vya kulelea watoto na maeneo mengine yenye mikusanyiko ya watoto.
“Kampeni yetu tutakwenda nyumba kwa
nyumba. Yaani mtoto alipo na sisi tutakwenda, tunakwenda na ile ile dhana ya
kuhakikisha hakuna mtoto tunamwacha, wananchi hawapaswi kusubiri timu za chanjo
ziwafikie majumbani pekee, bali wanapaswa kujitokeza katika vituo vya kutolea
huduma za afya watakaposikia zoezi hilo linafanyika katika maeneo yao,” alisema
Dkt. Sebastian.
Aidha, alisema kuwa mwitikio wa
wananchi katika maandalizi ya kampeni hiyo umekuwa mzuri, akiwashukuru wananchi
kwa ushirikiano wao.
Akiongelea maandalizi, aliyataja kuwa yamehusisha
viongozi katika ngazi mbalimbali, kuanzia wilaya, tarafa, kata hadi mitaa, ili
kuhakikisha taarifa kuhusu kampeni hiyo inawafikia wananchi wote.
Akiongelea usalama wa chanjo hiyo,
aliwahakikishia kuwa chanjo inayotolewa ni salama na kuwataka kuwa na amani na
kuendelea kupata ufafanuzi kutoka kwa wataalamu wa afya pale wanapokuwa na
maswali.
Kampeni ya chanjo ya Polio inatarajiwa
kufanyika tarehe 27-30 Agosti, 2026,
huku wataalamu wa afya wakisisitizwa umuhimu wa wazazi na walezi kuhakikisha
watoto wanapata chanjo hiyo kwa ajili ya kuwalinda dhidi ya ugonjwa wa Polio.
Comments
Post a Comment